Na IRENE MWASOMOLA
CHAMA cha Wakandarasi Wanawake Tanzania (TWCA), kimeeleza mambo manane waliyofanikiwa chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Mojawapo ni kuandika historia ya kutekeleza miradi zaidi ya 300 katika kipindi cha miaka mitatu.
Pia, kimesema chini ya Rais Dk. Samia, wamefanikiwa kutekeleza mradi wa barabara ya kilometa 20 ya Ruanda Idiwili mkoani Songwe wenye thamani ya sh. bilioni 45.
Akizungumza na UHURU, Rais wa TWCA, Mhandisi Dk. Judith Odunga, amesema hatua ya kuaminiwa kutekeleza mradi wa barabara ya Ruanda Idiwili, ni jambo la kihistoria kwa kuwa, halikuwahi kutokea kabla ya hapo.
Dk. Judith, ametaja jambo la tatu walilofanikiwa chini ya Rais Dk. Samia, ni kupata fursa mbalimbali za kushiriki zabuni zinazotolewa katika mikoa.
“Chini ya Rais Dk. Samia, tumefanikiwa kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa ukiwemo wa Ruanda Idiwili wenye thamani ya sh. bilioni 45 wa kilometa 20.
“Kwetu ni historia, haijawahi kutokea, zamani tulikuwa tunapata miradi midogo midogo ya milioni 300,” alisema.
Aidha, Mhandisi Dk. Judith, amesema jambo la nne wanalojivunia ni serikali kuja na sera inayoelekeza asilimia 30 ya miradi itekelezwe na wanawake, hatua hiyo inawasaidia kufanya vizuri na kushiriki kikamilifu katika sekta ya ujenzi na maendeleo kwa ujumla.
Tano, Mhandisi Dk. Judith, amesema TWCA ,imefanikiwa kutoa mafunzo kwa wasichana wanaosomea uhandisi katika vyuo mbalimbali nchini.
Pia, amesema jambo la sita walilofanikiwa chini ya uongozi wa Rais Samia, ni kupata mikopo kirahisi kupitia taasisi za fedha.
Vilevile Dk. Judith, ametaja mafanikio ya saba wanayojivunia ni kuwezesha wasichana wanaosomea uhandisi, kufungua kampuni za awali za ukandarasi.
Kwa mujibu wa Dk. Judith, TWCA imefanikiwa kupata fursa ya kushirikiana na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), kutoa mafunzo ya uhandisi.
KATIBU MKUU TWCA
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa TWCA, Mhandisi Deborah Sengati, alisema kupitia utekelezaji wa mradi wa barabara ya Ruanda, serikali iliwawezesha kupata malipo ya awali ya mradi kwa haraka na kulegeza baadhi ya masharti.
Mhandisi Deborah, alimshukuru Rais Samia kwa dhamira njema aliyonayo kuwainua wanawake kiuchumi, huku akisema TWCA, inajivunia mafanikio chini uongozi wake.
Alisema kupitia ushirikiano wa serikali, TWCA imeunganisha wakandarasi wanawake, kuwajengea uwezo na kuwapatia elimu ya matumizi ya fedha.
“TWCA tumejenga mahusiano mazuri na benki, sasa taasisi mbalimbali zimelegeza masharti tunaweza kupata mikopo kirahisi,” aliongeza.
TWCA ilianzishwa Aprili 11, mwaka 2019, kikiwa na lengo la kuunganisha wakandarasi wanawake kwa lengo la kutafuta fursa mbalimbali serikalini.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega alizindua barabara inayojengwa na wakandarasi wanawake ya Ruanda Idiwili, huku akisema Rais Dk. Samia amefanya uamuzi wa kimkakati wa kuinua wanawake katika sekta ya ujenzi.
Ulega alisema kwa muda mrefu wanawake walitumika katika shughuli za kusafisha barabara, lakini chini ya Rais Dk. Samia mageuzi makubwa yamefanyika ambayo yamewaongezea fursa na heshima.




