Na IRENE MWASOMOLA
MWANASIASA mkongwe Mzee Paul Kimiti na Mwenyekiti mstaafu wa Chama cha ADC, Hamad Rashid, wametoa rai kwa Watanzania kuwapuuza baadhi ya watu wanaochochea wananchi wasitoe maoni katika Tume ya Rais ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani Oktoba 29.
Wamesema kuundwa kwa tume hiyo ni wajibu wa kikatiba, hivyo wanaohamasisha wananchi wasitoe ushirikiano kwa tume hiyo hawalitakii mema Taifa.
Kauli hizo zimekuja ikiwa imepita siku moja tangu Tume ya Rais ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi, kubaini uwepo wa watu wanaoshawishi wananchi kutotoa ushirikiano.
Akizungumza na UHURU, Hamad Rashid alisema ni wajibu wa Watanzania kutoa ushirikiano kwa tume hiyo, kwani si mara ya kwanza serikali kuunda tume, ambapo mwaka 2001 Rais wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin Mkapa aliunda kwa ajili ya kuchunguza vurugu Zanzibar.
“Matukio ya Oktoba 29 hakuna aliyefurahia, hivyo kuundwa kwa tume ni wajibu wa kikatiba, niwaombe Watanzania wawapuuze watu ambao halitakii mema Taifa letu, wawapuuze wale wote wanaochochea wananchi wasishiriki kutoa maoni,” alisema.
Kwa mujibu wa Rashid, watu wanaoshawishi wananchi wasishiriki kutoa maoni wanaweza kuwa wanahusika na vurugu hizo na wanapaswa kufuatiliwa.
Mwanasiasa mkongwe na kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mzee Kimiti, aliwataka wananchi kushiriki kikamilifu kutoa maoni kwa tume hiyo ili iweze kukamilisha uchunguzi wake.
Kauli ya Tume
Desema 26 mwaka huu Tume ya Rais ya kuchunguza matukio ya vurugu wakati na baada ya uchaguzi, ilisema imebaini kuwepo kwa watu au makundi ya watu yanayoshawishi wananchi kutotoa ushirikiano, ikiwemo kutoa maoni, ushahidi au taarifa kwa namna yoyote ile.
Taarifa hiyo ilisema ushawishi huo hausaidii jitihada za kitaifa za kutafuta ukweli, haki, kujifunza kutokana na yaliyopita na kuweka misingi ya suluhu ya kudumu.
Iliwashauri wananchi kupuuza ushawishi wowote unaolenga kuwazuia kushiriki, badala yake watoe maoni.
“Kupitia sauti za wananchi, Taifa linaweza kutambua changamoto zilizojitokeza, kuzitatua na kuchukua hatua za kuhakikisha matukio kama haya hayajirudii siku zijazo,” ilisema taarifa hiyo.
Pia taarifa hiyo ilifafanua kwamba tume hiyo ipo kwa ajili ya Watanzania wote na mafanikio ya kazi yake yanategemea ushiriki mpana, wa hiyari na wenye uwazi kwa wananchi.
Novemba 18 mwaka huu, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, aliunda tume hiyo baada ya kutokea kwa vurugu na uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi mkuu Oktoba 29.
Hatua hiyo ilikuwa ni utekelezaji wa ahadi aliyotoa wakati akihutubia Bunge la 13 Jijini Dodoma, ambapo aliahidi kuunda tume huru ya kuchunguza tukio hilo.
Tume hiyo inaongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu Othuman Chande, wajumbe wa tume hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Balozi Dk.Tergomena Tax, Jaji Mkuu Mstaafu Profesa Ibrahim Juma, Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu Balozi Ombeni Sefue.
Wengine ni Balozi Paul Meela, Balozi David Kapya, Mwanadiplomasia Balozi Radhia Msuya, Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu Said Mwema.




