Na WAANDISHI WETU
IDADI kubwa ya wananchi Mkoa wa Dar es Salaam, wamejitokeza kuchukua Vitambulisho vya Taifa (NIDA), huku chanzo cha watu wengi kujitokeza kikielezwa.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), James Kaji, aliwataka wananchi kwenda kuchukua vitambulisho vyao wilayani.
NIDA TEMEKE
Mwamko mkubwa wa wananchi kuchukua vitambulisho, umekuwa mkubwa katika Wilaya ya Temeke.
Akizungumza, Ofisa Msajili wa Wilaya ya Temeke, Mohamed Mpili, alisema hadi sasa vitambulisho 53,232, vimechukuliwa na wananchi kati ya 95,546.
Mpili, alisema awali NIDA ilikuwa ikipeleka vitambulisho ofisi za kata kuwarahisishia wananchi kuvipata.
Alieleza utaratibu huo, ulikuwa na nia njema ya kusaidia wananchi na kuwaondolea usumbufu wa kufuata huduma mbali.
Hata hivyo, ulisababisha changamoto kubwa kwa vitambulisho kubaki muda mrefu.
Alisema baadhi ya vitambulisho, viliachwa muda mrefu ofisi za kata na kusababisha baadhi kuharibika, kuungua au kupata msukosuko.
“Maelekezo yalitolewa ya kukusanya vitambulisho vyote vilivyokuwa katika kata na kuvipeleka Ofisi ya Wilaya ya Temeke, ambako vilifanyiwa upembuzi kwa lengo la kubaini vilivyoharibika na salama,” alieleza Mpili.
Mpili, alisema vitambulisho vilivyoharibika vilirejeshwa kufanyiwa marekebisho na uchakataji upya na vilivyo safi, viliendelea kuandaliwa kwa matumizi.
Baada ya zoezi hilo, ofisi ya wilaya, ilianza mchakato wa kuvisomesha vitambulisho kwa kutumia namba za usajili za wananchi, iliwezesha kupata ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) wa kuitwa kuchukua.
Alisema awamu ya kwanza ya ujumbe huo, ilisababisha mwitikio mkubwa, ambapo kwa siku wananchi kati ya 400 hadi 700 walichukua vitambulisho.
Alieleza kuwa, awamu hiyo ya pili, ofisi ya wilaya iliweka mahema kutokana na wingi wa wananchi, huku zaidi ya watu 1,000 wakihudumiwa kwa siku na kati ya 700 hadi 800, wakivichukua.
Alibainisha hatua ya kufungiwa huduma ilikuwa chachu kubwa iliyowasukuma wananchi wengi kuchukua vitambulisho vyao.
Mpili alisema hivi sasa wananchi wanaofika kuchukua vitambulisho imepungua ni watu kati ya 100-150, baada ya wengi kuchukua.
Kwa upande wa usajili, Mpili alisema ofisi imerahisisha upatikanaji wa fomu za NIDA kupitia mtandao, na kuandaa mipango ya usajili wa jumla katika kata kubwa kuweka kambi.
“Katika usajili wa jumla tuna mkakati wa kwenda kata sita za Temeke kuweka kambi ya siku 20 Januari mwakani, lengo ni kurahisisha upatikanaji wa huduma.
“Kambi hiyo tunatarajia kuifanya kata zenye idadi kubwa ya watu kama Mbagala, Buza, Yombo Vituka na maeneo mengine ya Temeke,”alisema.
NIDA KINONDONI
Zaidi ya watu 150 wanakwenda huchukua vitambulisho kila siku wilayani Kinondoni, hatua inayodhihirisha kuongezeka mwamko wa wananchi.
Ofisa Usajili wa Wilaya ya Kinondoni, Irene Mn’gon’go, alisema wastani wa wananchi 150 huchukua vitambulisho kwa matumizi ya kiofisi na kijamii.
Irene alisema mwaka huu, wananchi 153,118 walichukua vitambulisho vyao, huku vitambulisho takribani 7,000 vikiwa havijachukuliwa na wahusika wake.
Aleleza ongezeko hilo limetokana kwa kiasi kikubwa na tangazo la NIDA kufungia matumizi ya namba za NIDA ambazo hazijaunganishwa na vitambulisho halisi.
Irene alisema kuanzia Mei mwaka huu, NIDA ilisitisha matumizi ya namba zote za NIDA zisizo na vitambulisho, hatua iliyolenga kuhimiza wananchi kuchukua vitambulisho vyao.
Alisema utekelezaji wa agizo hilo umechochea wananchi kujitokeza kwa wingi kuchukua vitambulisho ambavyo awali vilikuwa havichukuliwi.
“Awali hali ilikuwa tofauti kwa siku unaweza usipate hata mtu anayekuja kuchukua kitambulisho chake, lakini kwa sasa idadi imeongezeka. Hii inaonyesha kuwa tangazo la Mkurugenzi Mkuu limetekelezwa kikamilifu,” alisema Irene.
Aliongeza awali vitambulisho hivyo vilikuwa vikipelekwa katika ngazi ya kata, kurahisisha wananchi kuvichukua haraka.
“Hata hivyo, tulibaini uchukuaji katika ngazi ya kata ulikuwa unasuasua na baadhi ya vitambulisho vilikuwa havionekani, jambo lililotulazimu kulirudisha zoezi hili mikononi mwa wilaya,” alisema.
Alisema tangu zoezi hilo lirudishwe wilayani, uchukuaji wa vitambulisho umeimarika na kuendelea vizuri, huku udhibiti na ufuatiliaji ukiwa wa karibu.
Alisema kasi ya uchukuaji imeongezeka kutokana na ukweli kuwa huduma nyingi muhimu mtu hawezi kupata bila kuwa na Kitambulisho cha NIDA.
Alifafanua miongoni mwa huduma hizo ni usajili wa laini za simu za mkononi, uandikishaji wa watoto shuleni, upatikanaji wa hati za kusafiria, mikopo mbalimbali, pamoja na huduma za bima ya afya.
“Hivi sasa NIDA imekuwa kama maji, huwezi kuyaepuka. Ukikosa kutumia huduma hii upande mmoja, utakutana nayo upande mwingine. Hivyo ni muhimu wananchi wajitokeze kwa wingi kuchukua vitambulisho vyao,” alisema.
Alitoa wito kwa wananchi ambao bado hawana vitambulisho vya NIDA kuweka mikakati ya haraka ya kuvipata, akisisitiza Kitambulisho cha Taifa ni nyenzo muhimu katika maisha.
NIDA ILALA
Kaimu Ofisa Usajilii wa NIDA Wilaya ya Ilala, Boniface Mango, aliwataka wananchi waliotumiwa ujumbe kwenda kufuata vitambulisho vyao.
Mango alisema mwamko wa wananchi kufuata vitambulisho vyao ofisini hapo baada kurejeshwa kutoka ofisi za kata ni mzuri.
Mango alisema baada vitambulisho hivyo kurejeshwa kutoka ofisi za kata, vilisomeshwa upya katika mfumo na wahusika walitumiwa ujumbe wa kufuata.
Alisema kwa sasa mwitikio wa wananchi kwenda kufuata vitambulisho ofisini hapo ni mkubwa na huenda inasababishwa na baadhi ya taasisi kutaka vitambulisho.
“Mwitikio wa uchukuaji vitambulisho ni mkubwa ukilinganisha na awali, huenda kwasababu baadhi ya ofisi wanalazimisha kitambulisho hicho, na hii ni kwasababu ya mifumo kusomana,” alisema Mango.
“Ni nadra sana mfumo unapokutumia ujumbe wa kufuata kimbulisho na uende sehemu husika ukikose
“Tunawaruhusu wananchi waje kwa wingi waulize, mwananchi mwenye namba ya NIDA anaitumia ikatokea amepata changamoto aje ofisini tutaangalia mfumo wetu na kutoa majibu sahihi,”alisema.
April 14, mwaka huu, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ilitangaza kuanzia Mei Mosi, mwaka huu, itasitisha rasmi matumizi ya Namba ya Utambulisho wa Taifa (NIN) kwa watu wote ambao hawajajitokeza kuchukua vitambulisho vyao licha ya kupewa taarifa kwa njia ya ujumbe mfupi wa maandishi (SMS).
Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Kaji alisema kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha kila kitambulisho kilichozalishwa na kugharimiwa kwa fedha za umma, kinatumiwa na mhusika aliyesajiliwa kihalali.
“Mtu ambaye hajajitokeza kuchukua kitambulisho chake licha ya kupokea SMS kutoka NIDA, kuanzia Mei Mosi 2025 hataweza tena kutumia NIDA yake kupata huduma yoyote,” alisema Kaji.
Kaji alisema uamuzi huo huwahusu ambao hawajapokea ujumbe wa SMS unaowataka kwenda kuchukua vitambulisho vyao.
Kaji alisema kuwa tayari vitambulisho vingi vilivyokamilika vilisambazwa katika ngazi za serikali za mitaa, kata, vijiji na shehia,kuwarahisishia wananchi kuvichukua karibu na maeneo yao ya makazi.
Habari na Athnath Mkiramweni, Rehema Maigala na Rehema Mohamed.




