VATICAN CITY, Vatican
WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabiti Kombo amewasilisha ujumbe maalumu wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Leo XIV.
Barua hiyo ya Rais Dk. Samia kwa Papa Leo iliwasilishwa na Waziri Kombo katika ziara rasmi ya kiserikali aliyoifanya Vatican akiwa pamoja na viongozi wengine wa serikali akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi Maalumu, Profesa Palamagamba Kabudi.
Katika kuwasilisha ujumbe wa Rais, Waziri Kombo amemuomba Papa Leo aiombee amani Tanzania baada ya vurugu za Oktoba 29. Waziri Kombo na ujumbe wake ulikutana na Arch Bishop Paul Gallagher, Waziri wa Mambo ya Nje wa Vatican.
Waziri Kombo alimweleza Arch Bishop dhamira ya Tanzania kufungua ubalozi Vatican. Kwa sasa Tanzania inawakilishwa kutokea Ujerumani.
Wasomi, wanadiplomasia wapongeza
Wasomi na wanadiplomasia nchini wamesema wametoa maoni tofauti baada ya Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Papa Leo XIV kukutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiriano wa Afrika Mashariki, Balozi Kombo.
Balozi Christopher Liundi, alisema ujumbe uliotumwa kwa Papa Leo XIV umeleta tija kwa taifa na imeonesha uwezo wa Tanzania wa kutofungamana na upande wowote.
“Kwasababu msingi ni masuala ya amani, ujumbe huo unaleta tija kwa taifa letu, ni kheri na fanaka ni faida kwetu, inaonesha uwezo wetu wa kutofungamana upande wowote,”alisema Balozi Liundi.
Kwa upande wake Mchambuzi wa diplomasia na masuala ya kimataifa, Gerson Mgonja, alisema kitendo Rais Dk. Samia, kutuma ujumbe Vatican unaonesha dunia kwa vitendo kwamba yeye ni bingwa wa diplomasia.
Kwa mujibu wa Mgonja, kupitia ushirikiano huo Watanzania wanaoishi Vatican, wanahakikishiwa uhusiano mzuri na ushirikiano bora katika ubalozi.
Pia, alisema hatua hiyo inaweka mazingira bora kwa wafanyabiashara wa nchi zote mbili kutekeleza shughuli zao kutokana na kuondolewa vikwazo mbalimbali.
Mhadhiri wa diplomasia kutoka Kituo cha Uhusiano wa Kimataifa cha Dk. Salim Ahmed Salim, Dk. Denis Konga alisema, ujumbe wa Rais Dk. Samia kwa Papa Leo XIV unaonesha namna Tanzania inatambua mchango mkubwa wa viongozi wa dini wa kimataifa.
Pia, Dk. Konga alisema hatua hiyo inaonesha namna gani utengamano wa kitaifa ni muhimu.
Naye Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Dk. Philip Daninga, alisema kidiplomasia hatua hiyo itaimarisha uhusiano wa kijamii, kiuchumi na kimataifa.
Dk. Daninga aliongeza kuwa, ujumbe wa Rais Dk. Samia kwa Papa Leo XIV unaleta tafsiri kwamba Tanzania ni nchi inayokaribisha ushirikiano na mataifa mbalimbali katika nyanja tofauti tofauti.




