Na NASRA KITANA
WAKATI timu ya Yanga ikitarajiwa kushuka dimbani kesho katika mchezo wa marudiano dhidi ya Al Ahly, uongozi wa Yanga umeweka wazi kuwa huo ni mchezo wao wa maamuzi, hivyo hawatakubali kupoteza.
Yanga wanatarajiwa kushuka dimbani kesho katika mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), dhidi ya Al Ahly ya Misri, utakaochezwa Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar kuanzia saa 10:00 jioni.
Timu hiyo yenye maskani yake Mtaa wa Twiga na Jangwani, itashuka dimbani huku ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza 2-0 katika mechi iliyopita iliyofanyika Uwanja wa Al Salam, Cairo, Misri.
Akizungumza kuelekea mchezo huo, Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe alisema mechi hiyo ndiyo itatoa maamuzi ya timu yao kusonga mbele katika hatua ya robo fainali ya CAFCL.
Alisema kuwa walipoteza ugenini, hivyo hawatakubali kupoteza nyumbani kwani watapambana kwa kila hali kuhakikisha wanaibuka na ushindi.
Kamwe alisema kuwa wachezaji wote wapo tayari na wana morari ya kutosha kuelekea katika mchezo huo na kila mmoja ameahidi kupambana na kutimiza majukumu yake uwanjani.
“Huu ni mchezo wetu wa maamuzi, tunahitaji kupata ushindi kwa namna yoyo ili kujihakikishia nafasi ya kutinga robo fainali ya CAFCL msimu huu,” alisema Kamwe.
Kamwe alisema benchi la ufundi limeona makosa waliyofanya katika mechi iliyopita na kuyafanyia kazi kuhakikisha wanaibuka na ushindi wakiwa uwanja wa nyumbani na kuwapa raha mashabiki wao.
Alisema kikosi tayari kilishawasili Zanzibar kuhakikisha wanafanya maandalizi ya mwisho kabla ya mchezo huo.
Hata hivyo aliwaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi kuhakikisha wanawapa sapoti wachezaji wao ili kuibuka na ushindi.
“Mashabiki ndio nguzo muhimu katika mchezo wetu na Al Ahly, kwani watawaongezea morari wachezaji ili kupata ushindi, tunawaomba wajitokeze kwa wingi,” alisema.
Katika msimamo wa kundi B, Yanga inashika nafasi ya pili kwa pointi nne Al Ahly ipo kileleni kwa pointi saba, AS FAR ikishika nafasi ya tatu kwa pointi mbili sawa na JS Kabylie inayoburuza mkia, timu zote zimeshashuka dimbani mara tatu.




