Na ANGELA SEBASTIAN,
Bukoba
MAKAMU wa Rais Balozi, Dk.Emmanuel Nchimbi, amemwagiza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, kutatua changamoto ya fedha za ujenzi wa bweni la wavulana na nyumba za walimu kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) tawi la Kagera.
Balozi Dk. Nchimbi, alieleza hayo mjini hapa, alipoweka jiwe la msingi la ujenzi unaoendelea wa majengo ya tawi la chuo hicho katika vijiji vya Itahwa na Kangabusharo wilayani Bukoba.
Alisema ujenzi huo uliopo chini ya Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mabadiliko ya Kiuchumi (HEET), unatekelekelezwa mikoa yote nchi nzima.
Alisema lengo ni kuwezesha idadi kubwa ya vijana wanapata elimu yenye ubora na ujuzi wa kuwakwamua kiuchumi.
“Ujenzi wa chuo hiki ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kukuza uchumi na kuchochea maendeleo ya Mkoa wa Kagera na taifa, lengo ni kuhakikisha kila mkoa unapata tawi la chuo kikuu,”alisema Balozi Dk. Nchimbi.
Aidha, Balozi Dk. Nchimbi, aliagiza uongozi wa chuo hicho, kuhakikisha mitaala inayotolewa inaendana na utolewaji elimu ya amali ya kuwawezesha wanafunzi kujiajiri baada ya kuhitimu.

Makamu wa Rais, alisema serikali itatekeleza maombi ya ujenzi wa mindombinu ya barabara zinazozunguka chuo hicho kwa kiwango cha lami ili kukipa hadhi chuo.
Naye Mkuu wa Chuo, Rais mstaafu Jakaya Kikwete, alisema chuo hicho, kitachochea kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi kwa wananchi wa Kagera.
Kikwete, alisema Rais Samia amejibu ombi la wananchi wa Kagera kutaka mkoa huo kuwa na chuo kikuu cha kuendelea kuzalisha wasomi wengi.
Aliwataka viongozi wa Kagera, kuongeza ukubwa wa eneo jingine nje ya lililopo, kwa ujenzi endelevu kwa sababu, mkakati ni kuhakikisha tawi hilo linakuwa Chuo Kikuu kinachojitegemea.




