Na MWANDISHI WETU
SERIKALI imewatangaza wanafunzi 50 bora waliofanya vizuri katika mtihani wa Kidato cha Sita mwaka 2026, watakaopelekwa kusoma nje ya nchi katika fani za Akili Unde (AI), Data Science na teknolojia nyingine za kisasa kupitia mpango wa Samia Scholarship.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameyasema hayo leo Julai 27, 2026 jijini Dodoma, wakati akitangaza orodha ya wanufaika wa mpango huo.
Prof. Mkenda amesema, jumla ya wanafunzi 1,050 watanufaika na Samia Scholarship, ambapo wanafunzi 1,000 watasoma katika vyuo vikuu vya ndani huku 50 bora zaidi wakipata nafasi ya kusoma nje ya nchi.
Amesema mpango huo unatekelezwa kwa maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuibua na kuendeleza vipaji katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM), ili kuzalisha wataalamu watakaochochea maendeleo ya taifa.
Aidha, amesema wanafunzi watakaopata ufadhili wa ndani wanapaswa kuomba udahili katika vyuo vikuu vya Tanzania katika shahada za Hisabati, Sayansi, Uhandisi au Tiba, kisha kujaza fomu ya kujiunga rasmi na mpango wa Samia Scholarship, ambapo serikali itagharamia masomo yao kwa asilimia 100.
Wanafunzi hao wametokana na tahasusi za PCM, PCB, CBG, PMG, CBA na PMC.



