Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso, ametoa maagizo ya mgawo wa maji kuwa shirikishi kwa kuwahusisha viongozi wa mitaa, nyumba na wilaya kuhakikisha ratiba ya upatikanaji wa maji inatekelezwa kwa ufanisi.
Aweso alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam, katika kikao kazi na Meneja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) aliowaagiza katika kipindi hiki cha mpito wa upungufu wa huduma ya maji uliojitokeza, wahakikishe ratiba ya mgawo inafika maeneo yote na maji yawe yanatoka siku nzima.
Alisema ushirikishwaji huo ni muhimu kwa sababu viongozi wa ngazi za chini wanafahamu kwa undani hali halisi ya upatikanaji wa maji katika maeneo yao.
Waziri Aweso alisema kupitia ushiriki wa viongozi hao, inakuwa rahisi kufuatilia utekelezaji wa ratiba na kubaini maeneo ambayo hayajapata huduma kama ilivyopangwa.
Alieleza ratiba ya mgawo wa maji inapaswa kuwa wazi, wananchi wafahamu siku na muda watakaopata huduma, hatua itakayowapa nafasi ya kujiandaa mapema badala ya maji kuja ghafla na kuondoka bila manufaa.
Akitoa mfano wa maeneo ya Ubungo, Kimara, Mwananyamala, Manzese hadi Kinondoni, Aweso alisisitiza endapo ratiba itaonesha uwazi huduma ya maji itapatikana siku fulani, lazima timu za mamlaka husika ziwepo kuhakikisha maji yanawafikia wananchi kama ilivyoelekezwa.
Alisema ratiba ya maji lazima iendane na utekelezaji halisi na kujenga imani kwa wananchi.
Aidha, alielekeza Jiji la Dar es Salaam na Pwani kugawana kanda za mgawo wa maji kupunguza mzigo wa kusambaza huduma katika maeneo mengi kwa wakati mmoja.
“Kwa kufanya hivyo, kanda husika zitapatiwa maji muda mrefu zaidi badala ya huduma ya muda mfupi isiyokidhi mahitaji ya wananchi,” alisema.
Alisisitiza kumpatia mwananchi maji kwa siku nzima kunamwezesha kuhifadhi maji kwa matumizi ya siku kadhaa.
Kwa mujibu wa Aweso, mgawo wa maji usio na ratiba ya uwazi na unaotokea dakika chache hauna tija, hivyo kuagiza kuendelea kuboresha ratiba za upatikanaji maji, wananchi waelewe maana halisi ya ratiba hizo.
Juzi, Waziri Aweso katika mkutano kati ya DAWASA na wahariri wa vyombo vya habari wa kuzungumzia hali ya upatikanaji wa maji mkoani Dar es Salaam, aliitaka DAWASA kugawa maji kwa usawa, uwazi na kutoa ratiba, muda kwa eneo litakopata maji wananchi wapate muda wa kujiandaa.
“Ni wazi kuna vitu vingine viko nje ya uwezo wetu ikiwemo kuchelewa kunyesha mvua za vuli, niwaombe wananchi tuendelee kuwa na mshikamano katika kipindi hiki cha mpito.
“Nasisitiza DAWASA hiki kilichopo au tunachozalisha gaweni maji hayo kwa usawa na uwazi kwa kueleza katika ratiba zenu ni saa ngapi maji yatatoka katika eneo linalokusudiwa huduma hiyo, wananchi wajiandaa kupokea maji, kwa kufanya hivyo itapunguza malalamiko,” alisema.
Aliongeza jambo hilo liwe shirikishi kwa watu wote ikiwemo wadau wa sekta binafsi watengeneze namna nzuri ya kugawa maji kwa kushirikiana na DAWASA katika visima vilivyochimbwa pamoja na kuielimisha jamii namna ya kutunza vyanzo vya maji na kulinda mazingira.




