Na MWANDISHI WETU
BAADA ya Yanga kushindwa kutinga hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika,uongozi wa klabu hiyo umesema umejifunza mambo mengi katika michuano hiyo.
Yanga ilishinda mabao 3-0 dhidi ya JS Kabylie mchezo wa hatua ya makundi uliofanyika katika Uwanja wa New Amaan Complex, visiwaani Zanzibar.
Akizungumza baada ya kumalizika mchezo huo, Ofisa Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ally Kamwe alisema wataenda kupiga hesabu zao vizuri ili msimu ujao isitokee tena.
“Hii hali inaumiza kabisa asikwambie mtu unashinda mabao 3-0, halafu unasubiri matokeo ya timu nyingine kiukweli unatamani kulia kutokana na aina ya matokeo hayo,” alisema.
Ofisa huyo alisema mbali ya matokeo hayo, amekiri wachezaji wao walipambana na kuonesha kiwango bora ambacho kimewavutia mashabiki wa timu hiyo.
“Tumetoa jasho letu katika kundi ambalo lilionekana ni kundi la kifo, tunashukuru Mungu tumekusanya pointi nane lakini haikuwa bahati tumeshindwa kupata pointi nyingi za kuendelea robo fainali.
“Nawapongeza wachezaji wetu wamejituma sana siku ya mchezo, wamejitoa sana wamefanya kile ambacho wana Yanga walikitaka kwa kufunga mabao matatu, lakini mabao hayo hayatoshi maana mechi nyingine timu zilitoka sare,” alisema.
Ofisa huyo alisema wacezaji wao walipambana sana na kuonyesha kiwango kikubwa.
“Hizi pointi tulizovuna michuano hii tunajiona kabisa msimu ujao tuna uwezo wa kufika mbali zaidi, pia kila shabiki wa Yanga ameondoka uwanjani akiwa na furaha kutokana na kiwango bora ambacho wachezaji walionyesha,” alisema.
Ofisa huyo alisema hasira zao za kushindwa kutinga robo fainali wanaenda kuzimalizia katika Ligi Kuu Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho (FA).
“Mechi ya Kariakoo dabi ambayo itafanyika Machi Mosi, mwaka huu itafanyika dimba la New Amaan Complex hivyo tutakutana hapa siku hiyo kutakuwa na mambo mengi ambayo watu wataona hasira zetu,” alisema.




