Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali imetoa sh. trilioni 3.5 kufikia mwaka 2024 kwa uwezeshaji wa vijana kiuchumi kutoka sh. bilioni 904 mwaka 2021.
Amesema fedha hizo zimewasaidia vijana kupata mitaji ambayo imewawezesha kushiriki shughuli mbalimbali za uzalishaji mali na hatimaye kuinua vipato vyao na uchumi wa Taifa.
Majaliwa alieleza hayo, katika maadhimisho ya Wiki ya Vijana Kitaifa yaliyofanyika mkoani Mbeya. Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni ‘Nguvu Kazi ya Vijana kwa Maendeleo Endelevu.’
Alieleza kwamba, serikali imefanya hivyo kwa kutambua vijana ni nguvu kazi na ndiyo msingi wa safari ya maendeleo ya taifa.
“Vijana wakipewa nafasi na kuandaliwa ipasavyo, wanaweza kuwa nguzo kuu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kufanikisha Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs),” alisema.
Majaliwa aliongeza vijana wamekuwa nguzo muhimu ya maendeleo sekta mbalimbali nchini na wamechangia kwa kiwango kikubwa katika kilimo, biashara, teknolojia, michezo na sanaa.
“Katika nyanja za ubunifu na teknolojia, vijana ndiyo vinara wa matumizi ya teknolojia mpya na majukwaa ya kidijitali, ikiwemo Akili Mnemba (A1) na mifumo ya mawasiliano ya kisasa, michango yao imekuwa kichocheo cha mabadiliko chanya katika jamii na uchumi wa taifa,” alisema.
Alitoa wito kwa wadau wote kuhakikisha vijana wanashirikishwa kikamilifu ngazi zote za uamuzi, siyo tu kama wanufaika wa sera, bali pia kama wabunifu na viongozi wa mabadiliko ya kijamii na kiuchumi.
Akiwa katika banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Majaliwa alitoa wito kwa taasisi hiyo na wadau wengine wa elimu kuwapa kipaumbele cha mafunzo watu wenye ulemavu na kuwaandalia nyenzo muhimu za kujifunzia watumie ujuzi watakaoupata kuongezea kipato.
“Baada ya kutembelea banda hili nimejifunza kwamba, wapo vijana wenye ulemavu wana ujuzi na vipaji, wazazi tuwe tayari kuwatoa watoto wetu wenye ulemavu na taasisi za elimu ziwapokee na kuwapa ujuzi,” alisisitiza.
Kwa Upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Ridhiwani Kikwete alibainisha serikali inatambua umuhimu wa kundi la vijana, ndiyo maana inawekeza na kuthamini mchango na nguvu zao katika kuleta mabadiliko chanya kwa jamii.
“Hii ni rasilimali kubwa ambayo ikielekezwa na ikijengewa uwezo ipasavyo kupitia vipaji walivyonavyo italeta maendeleo endelevu, kujenga taifa shindani na lenye ustawi,” alisema.