Na SULEIMAN JONGO,
Bukoba
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amesema moja ya sharti la haki za binadamu ni kutowazuia wengine kupata haki yao ya kikatiba, ukiwemo upigaji kura kuchagua viongozi.
Amesema CCM, inaheshimu haki za binadamu, atakayeshindwa kuziheshimu na kusababisha uvunjifu wa sheria, atashughulikiwa kwa kadri sheria inavyoelekeza.
Pia, amewahakikishia Watanzania kuwa, kila mwenye sifa, atapata fursa ya kupiga kura kwa amani na utulivu na kwamba, hakuna yeyote atakayezuia Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, mwaka huu.
Wasira alisema hayo, alipozungumza na wanachama wa CCM kutoka Wilaya ya Bukoba, mkoani Kagera, akiwa katika ziara ya kumnadi Mgombea Urais, Dk. Samia Suluhu Hassan, wagombea ubunge na udiwani waliosimamishwa na Chama.
“Wenye matatizo madogo madogo, sisi tunawaambia wanazungumza sana, haki za binadamu na sisi tunawaambia tunaziheshimu, haki za binadamu zina masharti na masharti yake ni kwamba, kama unadai haki yako, wewe usiwazuie wengine kupata zao,” alisema.
Alisema kuwa, Dk. Samia ameahidi ndani ya siku 100 baada ya uchaguzi wa mwaka huu, ataanza kukaa pamoja na wanaohitaji kuzungumza naye kuhusu mambo wanayoona hayako sawa.
“Sisi hatujakataa kusikiliza hata kidogo, Dk. Samia amesema katika siku zake 100 baada ya uchaguzi, ataanza mjadala na wale ambao wanahitaji kuzungumza naye.
“Maana hatuendeshi nchi kwa mabavu, tunaendesha kwa mazungumzo.
“Kwa hiyo, kama kuna mmoja anafikiri yeye ana mawazo, lakini hayajasikilizwa bado nafasi ya kusikilizwa ipo, huwezi kusema utafanya fujo kwa sababu, hujasikilizwa, utashughulikiwa kwa sababu kuna kusikilizwa na kama hutaki kusikilizwa, unashughulikiwa walio wengi wapate amani, maana ni haki yao kupiga kura.
“Sheria zipo, zinasema watu wakienda kupiga kura, hakuna anayeruhusiwa kuwashawishi kimya au hata waziwazi kwamba, wasiende kupiga kura, anaingilia haki yao,” alieleza.
Kwa mujibu wa Wasira, kupiga kura ni haki ya kila mwananchi mwenye sifa, haipaswi kutumika vibaya kwa baadhi ya watu, kuwahadaa na kuwashurutisha wengine kutotimiza haki hiyo.
Wasira, alisema wapo baadhi ya watu wasioitakia mema CCM na nchi kwa ujumla, wanahoji kwa nini Chama kimemteua Dk. Samia kuwania nafasi hiyo na kwamba, jibu lao ni kuwa, hilo limefanyika kutokana na sifa na uwezo alionao kuongoza Watanzania.
“Sisi tumemchagua Samia kwa sababu, anakubalika na wananchi na ushahidi ni kupokelewa kila anakopita, hivi watu hao mlikuwa mnawaswaga na polisi kwenda kumpokea, si walikuwa wanakuja wenyewe?. “Kwa hiyo anayo sifa ya kukubalika, anayo sifa kubwa ya kusimamia utekelezaji wa maendeleo ya watu, hizo ndizo sababu zetu za msingi.




