Na MWANDISHI WETU
TIMU ya soka ya Taifa Stars inatarajiwa kutua nchini Morocco, keshokutwa kwa ajili ya kushiriki Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2025).
Kauli hiyo imetolewa jana na Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, Clifford Ndimbo alipozungumza na UHURU amesema kuwa kikosi kipo tayari kwa mashindano hayo.
“Kikosi cha Stars kitakwenda Alhamisi nchini Morocco, kikiwa kipo sawa sawa kwani wachezaji wote wana morali ya kutosha kuhakikisha wanaipambania nchi,” amesema.
Ndimbo ameongeza kuwa jana na leo wanatarajiwa wachezaji wote walioitwa wanaocheza soka la kulipwa Barani Ulaya watawasili kambini nchini Misri kabla ya kuanza safari ya Morocco.
Hata hivyo, Ndimbo amesema wachezaji wengine wote waliopo kambini nchini Misri wapo fiti na wanaendelea na programu za kocha wa timu hiyo, Miguel Gamondi.
Katika michuano ya AFCON 2025, timu ya Taifa Stars imepangwa na Kundi C n a timu za Nigeria, Tunisia na Uganda.
Katika mashindano hayo makubwa zaidi katika soka Afrika, timu zitakazoshiriki ni 24 ambazo ni Morocco, Mali, Zambia na Comoros, Misri, Afrika Kusini, Angola, Zimbabwe, Tanzania, Nigeria, Tunisia na Uganda.
Nyingine ni Senegal, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Benin, Botswana, Algeria, Burkina Faso, Guinea ya Ikweta, Sudan, Ivory Coast, Cameroon, Gabon na Msumbiji.
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), michuano ya AFCON inatarajiwa kutumia dau la dola za Marekani milioni 32 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 78.3 za Tanzania kwa ajili ya zawadi pekee.
Katika mchanganuo wa fedha hizo, bingwa wa michuano hiyo anatarajiwa kuvuna dola za Marekani milioni saba ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 17.1.
Timu itakayoshika nafasi ya pili itavuna dola za Marekani milioni nne ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 9.7 za Tanzania.
Timu mbili zitakazoishia hatua ya nusu fainali, kila moja itaondoka na dola za Marekani milioni 2.5 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 6.1 za Tanzania.
Timu nne zitakazoishia hatua ya robo fainali zitavuna dola za Marekani milioni 1.3 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 3.1 za Tanzania.
CAF pia imeeleza kwamba, miamba minane itakayoishia hatua ya 16 bora itavuna dola za Marekani 800,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.9 za Tanzania.
Timu zitakazoishia nafasi ya tatu katika kundi, kila moja itaondoka na dola za Marekani 700,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.7 wakati zile zitakazoburuta mkia katika kila kundi zitavuna dola za Marekani 500,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.2 za Tanzania.




