Na FRED ALFRED,
Dodoma
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma, imetoa siku 21 kwa wadaiwa wa viwanja 6,560 vyenye thamani ya sh. bilioni 55.4 vilivyopo maeneo ya Mtumba Zone II, Mtumba Zone III na Kikombo kujitokeza kufanya malipo.
Imesema watakaoshindwa kufanya hivyo, hatua zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kunyang’anywa kisha kurejeshwa sokoni.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dennis Gondwe, alisema hatua hiyo, imekuja baada ya halmashauri kukamilisha zoezi la uhakiki wa malipo ya viwanja na kubaini kuwepo kwa wadaiwa wengi wakiwemo watu binafsi, taasisi na kampuni.
Alisema kwa Mtumba Zone II pekee kuna viwanja 1,915 vyenye thamani ya sh. bilioni 28.8 ambavyo bado havijalipiwa kikamilifu, hali inayokosesha mapato Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Aidha, Mtumba Zone III ina viwanja 2,594 vyenye thamani ya sh. bilioni 20.6, huku eneo la Kikombo likiwa na viwanja 2,051 vyenye thamani ya sh. bilioni 5.9 na kufanya jumla ya thamani ya viwanja vyote kufikia sh. bilioni 55.4.
Gondwe, alisema ucheleweshaji wa malipo hayo umeathiri utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ukiwemo ujenzi na ukarabati wa barabara, upatikanaji wa maji safi na salama na usambazaji wa umeme.
“Mapato yatokanayo na mauzo ya viwanja ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa bajeti ya halmashauri, hususan kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi wa Jiji la Dodoma,” alisema.
Alisisitiza kuwa :”Wadaiwa wote wanapaswa kujitokeza ndani ya siku 21 kuanzia tarehe ya tangazo hilo ili kukamilisha malipo yao, vinginevyo hatua za kisheria zitachukuliwa ikiwemo kurejeshwa kwa viwanja hivyo sokoni.
Katika hatua nyingine, aliwataka wananchi waliokamilisha malipo lakini majina yao hayakuonekana katika orodha ya wadaiwa kufika katika ofisi za Jiji wakiwa na nyaraka halisi kwa ajili ya uhakiki.
Gondwe alibainisha kuwa lengo la zoezi hilo siyo kuwaadhibu wananchi, isipokuwa kuhakikisha uwazi, haki na upatikanaji wa rasilimali zitakazochochea maendeleo endelevu ya Jiji la Dodoma linalokuwa kwa kasi.




