Na MWANDISHI WETU
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amewahakikishia Watanzania kuwa, mkataba wa uboreshaji reli ya Tazara uliosainiwa kati ya Tanzania, Zambia na China, utaleta manufaa makubwa.
Manufaa hayo yatakuwa ya kiuchumi na kijamii kwa nchi, kinyume na madai yanayosambazwa na baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii, wakibeza hatua hiyo.
Akitoa ufafanuzi huo, Msigwa alisema reli ya Tazara ilijengwa kati ya mwaka 1970 na 1975 kwa mkopo usio na riba kutoka China na kukabidhiwa rasmi kwa Tanzania na Zambia mwaka 1976.
Hata hivyo, kwa miaka ya hivi karibuni, reli hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto kubwa za kiuendeshaji, hali iliyosababisha kushindwa kujiendesha kibiashara na kulazimu serikali kutumia fedha kuendelea kuihudumia bila tija inayostahili.
Alisema kuwa, kupitia mkataba mpya, Tanzania na Zambia, zimeingia makubaliano na China kupitia kampuni ya CCECC, ambapo China itawekeza dola za Marekani bilioni 1.4, sawa na zaidi ya sh. trilioni 3.45.
Alieleza kuwa, uwekezaji huo, unalenga kuboresha miundombinu ya reli ya Tazara, kujenga vituo vya kisasa, kununua treni za abiria na kujenga kituo kikubwa cha ‘Kidatu Trans shipment Joint Facility.’
Kituo hicho, kitawezesha mizigo kutoka reli ya kati yenye kiwango cha MGR, kuhamishiwa katika reli ya Tazara yenye kiwango cha Cape Gauge, hivyo kuongeza ufanisi wa usafirishaji.
Msigwa, aliongeza kusema pamoja na uboreshaji wa miundombinu, Kampuni ya CCECC, itatekeleza mradi huo kwa miaka mitatu na kuendesha reli ya Tazara kwa kipindi cha miaka 30.
Katika kipindi hicho, Serikali ya Tanzania, itakuwa inapokea Dola za Marekani milioni 30 kila mwaka, sawa na sh. bilioni 75, tofauti na hali ya sasa ambayo inalazimika kutoa zaidi ya sh. bilioni 28 kila mwaka kuchangia uendeshaji wa reli hiyo.
Kwa mujibu wa Msigwa, uwekezaji huo, unatarajiwa kuchochea kwa kiasi kikubwa uchumi wa Tanzania na Zambia, kwani reli ya Tazara itaunganishwa na mtandao wa reli za kiwango cha Cape Gauge zenye urefu wa zaidi ya kilometa 50,000 barani Afrika.
Alisema hatua hiyo itakuza masoko na kurahisisha biashara ya kikanda.
Alifafanua kuwa miongoni mwa manufaa makubwa kwa Tanzania ni kurahisisha usafirishaji madini mbalimbali yakiwemo ya ‘rare earth elements’, ‘cobalt,’ ‘granite,’ makaa ya mawe na chuma na mazao ya kilimo kwenda nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Msigwa, aliwataka Watanzania kupuuza kauli za kubeza uwekezaji huo mkubwa, akisisitiza mafanikio hayo, yametokana na juhudi za kidiplomasia za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Alieleza kuwa, Rais Dk. Samia, alikubaliana na Rais wa China, Xi Jinping kuhusu uwekezaji wa uboreshaji wa Tazara na kutoa wito kwa Serikali ya Zambia kukubali utekelezaji wa mradi huo, alipohutubia Bunge la nchi hiyo.
Hatua nyingine muhimu katika utekelezaji wa mradi huo ni kuzinduliwa rasmi kwa uboreshaji wa reli ya Tazara nchini Zambia uliofanywa na Waziri Mkuu wa China, Li Qiang.
Hatua hiyo, inayoashiria kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kimkakati kwa maendeleo ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.




