Na ABDURAHIM MZAKILU,(UDSM)
IKIBAKI siku moja kabla ya Yanga na Simba kuchuana katika Ngao ya Jamii, mchezo huo utakuwa na utamu wa kuwepo wa mastraika Peter Shalulile na Ibrahim Doumbia ambao wataongeza chachu ya ushindani wa miamba hiyo.
Huku uchungu ukiwepo kwa timu ambayo itapoteza mchezo huo ambao unasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki kuona nani atachukua Ngao hiyo ya jamii.
Yanga na Simba zitachuana kesho saa 2:30 usiku katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
UTAMU UKO HAPA
Katika pambano hilo, utamu utakuwepo kufuatia mwishoni mwa wiki makocha wa timu zote mbili, Steve Barker wa Simba na wa Yanga waliamua kuficha mbinu zao.
Makocha hao walitumia mfumo tofauti katika kipindi cha kwanza na kisha kutumia mfumo mwingine kipindi cha pili huku wakibadilisha wachezaji karibu wote.
Kabla ya kuchezwa pambano hilo na ujio wa msimu mpya, tayari utamu umeibuka kwa mashabiki kutaka kuona msimu ujao wachezaji Doumbia na Shalulile watafanya nini .
Kwani tayari nyota hao, wameingia kambani hatua inayoonyesha ni kwa kiasi gani nyota hao wapo fiti kuonyesha makali hasa katika dabi ya Kariakoo.
Doumbia alifunga bao la kwanza katika mechi ya makundi ya Kombe la CECAFA dhidi ya Singida Black Stars kabla ya kupachika lingine katika mechi ya kirafiki dhidi ya Al Merrikh ya Sudan.
Kwa upande wa Shalulile alifunga bao la kwanza akiwa na Yanga juzi katika mechi ya Yanga Day dhidi ya Aigles du Congo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Mastraika hao wawili wana nafasi kubwa ya kukutana kesho wakati timu zao zikichuana katika Ngao ya Jamii.
Yanga ni mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita wakati Simba ikiwa bingwa wa Kombe la FA 2026.
WACHAMBUZI, WACHEZAJI WA ZAMANI WAZUNGUMZA
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa hivi karibuni na baadhi ya wachambuzi wa soka nchini akiwemo Ramadhan Mbwaduke, zimeonesha kuwa Shalulile aliyekuwa Mamelodi Sundowns, amefunga mabao 130 katika mechi alizocheza nchini Afrika Kusini.
Pia, takwimu hizo zimeonesha kwamba Shalulile amewahi kuwa miongoni mwa wafungaji bora katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Nyota huyo alifanikiwa kufunga mabao sita katika msimu wa 2022/23.
Kwa upande wa mfumo wa uchezaji, Shalulile anaweza kutumika kama mshambuliaji wa kati katika mfumo wa 4-4-2, akitumia nguvu, kasi na uwezo wake wa kumalizia nafasi ya kupachika mabao.
Kwa upande wa Ibrahim Doumbia yeye amefanikiwa kupachika mabao 17 na kutoa pasi za kufunga mabao mara nne msimu uliopita nchini Mali.
Doumbia mwenye umri wa miaka 19, amesajiliwa na klabu ya Simba kutoka timu ya AS Korofina ya nchini Mali.
Mshambuliaji huyo anatajwa kucheza nafasi ya mshambuliaji, huku uwezo wake wa kufunga na kutengeneza nafasi kwa wenzake ukimfanya kuwa mchezaji muhimu katika safu ya mbele.
Mchezaji huyo imeelezwa kwamba ndani ya timu ya AS Korofina alikuwa anaweza kucheza mfumo wa 4-3-3 na kupiga mashuti langoni mwa timu pinzani.
Gwiji wa zamani wa Yanga, Mohammed Hussein ‘Mmachinga’, amesema nyota hao ni wachezaji wazuri lakini bado wanahitaji muda kuendana na mifumo ya vikosi vyao.
“Hawa wote ni wachezaji wazuri, ninachoamini wanahitaji muda tu kuzoea aina ya uchezaji wa timu kwa ajili ya kufanya makubwa,” alisema.
Mchezaji wa zamani wa Simba, Meddie Kagere, mwishoni mwa wiki alisema
anatamani kuiona Simba ikiendelea kuchukua mataji msimu mpya ikiwemo Ligi Kuu Tanzania Bara, Ngao ya Jamii na kufanya vizuri katika mashindano ya , Ligi ya Mabingwa Afrika.
“Nimeona usajili ni mzuri, wapewe muda watafanya vizuri ikiwemo kutwaa Ngao ya Jamii,”alisema nyota huyo.
WACHEZAJI
Hadi sasa, Yanga imesajili wachezaji 10 wapya ni Peter Shaulile kutoka Afrika Kusini , Cheikh Toure raia wa Ufaransa mwenye asıli ya Senegal.
Wengine ni Housseine Zakouani ambaye ni raia wa Comoro aliyezaliwa Ufaransa, Mzambia Albert Kangwanda, aliyeitumikia Red Arrows ya kwao na Fred Ngoma kutokea klabu ya Olympique de Safi ya Morocco.
Wachezaji wazawa sita ambao wamesajiliwa ni Juma Abushiri kutoka Fountain Gate, Hussein Mihambo (Mashujaa), Abdulnasir Muhamed (Mashujaa), Mohamed Mussa (Mashujaa), Erick Mwijage (Mashujaa) na Suleiman Mbarouk maarufu Mpemba D aliyekuwa JKU.
Kwa upande wa Simba msimu ujao, itakuwa na benchi la ufundi linaloongozwa na kocha Steve Barker.
Kikosi cha Simba kitakuwa na makipa ni Alexsendel Erasto, Abel Hussein, Yacoub Suleiman, Mamadou Kassali, Bashiru Kibaila, David Kameta ‘Duchu’, Vedatus Masinde, Nathaniel Chilambo, Antony Mligo, Ismail Toure, Wilson Nangu.
Wengine ni Hussein Mbegu, Abdulrazak Hamza, Nikson Kibabage, Rushine De Ruck, Shomari Kapombe, Yusuph Kagoma, Neo Maema, Moris Abraham, Ino Loemba, Kelvin Nashon, Hussein Semfuko, Libase Gueye, Bakari Msimu, Keletso Makgalwa, Anicet Oura, Ibraheem Jabaar,
Elie Mpanzu, Clatous Chama na Ibrahim Doumbia.
UCHUNGU
Timu zote mbili zitaingia uwanjani zikiwa na uchungu wa kufungwa katika matamasha yao.
Ikumbukwe kuwa Simba ilifungwa bao 1-0 na timu ya Polisi ya Kenya katika tamasha la Simba Day.
Yanga nayo ilipokea kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa timu ya Aigles du Congo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Mara ya mwisho timu za Simba na Yanga zilipambana Mei 3, mwaka huu ambapo zilitoka sare ya mabao 2-2.
Kutokana na hali hiyo, timu zote mbili zitaingia uwanjani kila mmoja akitaka kumfunga mwenzake na kusababisha pambano hilo kuwa na ushindani mkubwa hapo kesho.




