>>Ni agizo la Waziri Mkuu Dk. Mwigulu
>>Simbachawene asema maandamano ni haramu
Na IRENE MWASOMOLA
SERIKALI imewataka wananchi wasiokuwa na ulazima wa kutoka leo, watulie nyumbani.
Agizo hilo limetolewa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, alipowasilisha salamu za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan za maadhimisho ya miaka 64 ya Uhuru, ambapo aliwatakia Watanzania kheri.
Kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari, Waziri Mkuu alisema wananchi wasiokuwa na dharula washerehekee sikukuu hiyo nyumbani, isipokuwa ambao majukumu yao yanawataka kuwepo vituo vya kazi kama ambavyo wataelekezwa na viongozi wao.
Serikali imesema imejipanga kikamilifu na ipo imara, kudhibiti maandamano yaliyopangwa kufanyika leo katika mikoa mbalimbali nchini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, alisema Serikali haitambui maandamano hayo kwa kuwa hayana kibali rasmi.
Simbachawene alisema maandamano hayo yaliyohamasishwa mtandaoni, yana lengo la kuleta uvunjifu wa amani na kuchafua taswira ya nchi.
Hata hivyo, alisema vyombo vya ulinzi vimejipanga kikamilifu kudhibiti aina yoyote ya uhalifu, utakaofanyika kwa kisingizio cha maandamano hayo.
Simbachawene alisema kufuatia hali hiyo, aliwataka wananchi wasiokuwa na ulazima wa kutoka leo, kutulia nyumbani na alitoa tahadhari kwamba yeyote atakayeshiriki maandamano hayo atakumbana na vyombo vya ulinzi.
Aidha, waziri huyo aliwasisitiza wananchi kuepuka kuchungulia nje, badala yake wabaki ndani kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza endapo maandamano hayo yatafanyika.
“Maandamano hayo ni haramu hayaruhusiwi, hayana kibali na yako kinyume cha sheria. Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimejipanga kuyadhibiti.
“Kama hakuna ulazima sana wa wewe (mwananchi) kutoka kesho (leo) jizuie, kama hakuna ulazima kufanya ‘movement’ jizuie uangalie hali halisi inakwendaje,”alisema.
Alisema wanaohamasisha maandamano hayo na kudai ni ya amani hawajulikani, haifahamiki wataanzia wapi na yanalenga nini ingawa wanaoratibu wanaeleza yatakuwa makubwa kuliko yaliyotokea Oktoba 29, mwaka huu.
“Niwaombe wananchi wasithubutu kujitokeza, Oktoba 29 kuna wengine walijitokeza bila kujua wanachokimbilia ni kitu gani, walijikuta wamejiingiza katika jambo ambalo hawakulijua.
Tunaambiwa maandamano hayo ni makubwa kuliko yale ya Oktoba 29. Maandamano hayo ndiyo tuliyoshuhudia vituo vya mafuta vikichomwa, mali za watu zikiharibiwa, yale siyo maandamano ni mapinduzi,”alisema Simbachawene.
Waziri huyo aliwasihi wananchi kuendelea kuitunza tunu yta amani ambayo imedumu muda mrefu, hivyo aliitaka jamii kuimarisha umoja na mshikamano.
Desemba 2, mwaka huu akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam, Rais Dk. Samia alisema kilichofanyika Oktoba 29, hayakua maandamano badala yake yalikuwa na dhamira ya kupindua serikali.
Rais Dk. Samia alisema vurugu hizo siyo desturi au utamaduni wa taifa letu na kwamba vurugu zilizofanyika ni mradi mpana wenye ufadhili unaolenga kuchafua taswira ya nchi.
Wakati huo huo, akizungumza utaratibu wa ukamataji raia unaofanywa na baadhi ya askari wa Jeshi la Polisi, waziri huyo alisema amemwelekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Camillus Wambura, utumike utaratibu uliozoeleka usioleta hofu au vitisho kwa wananchi.
“Ukamataji ninaopenda ni ule wa kisheria, askari anaenda na sare anaripoti kwa mjumbe, yanini uende usiku umevaa ninja,”alisema.
Waziri Simbachawene alisema hakuna sababu ya ukamataji unaoleta hofu kwa wananchi, isipokuwa pale itakapobidi ufanyike kulingana na kosa.
Maandamano hayo yanaratibiwa mitandaoni zikiwa zimepita siku 42 tangu kutokea vurugu na uharibifu wa mali uliyofanywa Oktoba 29.




