Na FRED ALFRED, Dodoma
MAFANIKIO makubwa yameshuhudiwa katika sekta ya maendeleo ya jamii nchini ndani ya siku 100 tangu Rais Samia Suluhu Hassan, alipoingia madarakani ambapo neema sasa kuwashukia waendesha bodaboda, bajaji wafanyabiashara wadogo (wamachinga) mama na baba lishe.
Kama alivyaohidi Rais Dk. Samia katika mikutano yake ya kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 29 mwaka jana, pindi atakapoingia madarakani atatoa mikopo kwa wajasiriamali, ahadi hiyo imetimizwa baada ya serikali kutenga sh. bilioni 10 za awali ambazo watakopeshwa kwa masharti nafuu.
Hayo yalibainisha jijini hapa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Doroth Gwajima, alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio katika utambuzi, urasimishaji na uwezeshaji wajasiriamali ndani ya siku 100 tangu Rais Dk. Samia aliposhika hatamu kuliongoza Taifa.
“Wizara imesajili wafanyabiashara ndogondogo 119,595 katika Mfumo wa Usimamizi na usajili wa Wafanyabiashara Ndogondogo (WBN–MIS) waweze kunufaika na fursa za kiuchumi ambapo wanawake ni 73,341 na wanaume ni 46,254.
Aliongeza: “Katika usajili huo, machinga ni 103,102, Mama na Baba Lishe ni 12,384 na waendesha bodaboda na bajaji 4,109.”
Vilevile, alisema katika kipindi hicho, wizara imepokea sh. bilioni 10.5 za kutoa mikopo yenye masharti nafuu ya riba ya asilimia saba kwa mwaka.
Alisema hadi sasa sh. bilioni 1.3 zimetolewa kwa wafanyabiashara 588 kupitia mfumo wa Benki ya NMB huku utoaji mikopo unaendelea katika maeneo mbalimbali nchi.
Pia, alisema kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake, sh. milioni 337.9 zimetolewa kwa wanawake wajasiriamali 45 kwa riba ya asilimia nne.
USAJILI WAENDESHA BODABODA, BAJAJI
Dk. Gwajima, alisema kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), waendesha pikipiki na bajaji 209,632, wamerasimishwa kwa kupatiwa leseni za udereva.
Alibainisha kuwa, kupitia mfumo wa Wezesha Portal, vikundi 6,041 vya wajasiriamali vimetambuliwa na kusajiliwa, vikiwemo vikundi vya wanawake 3,207, vijana 2,318 na watu wenye ulemavu 516/
Kadhalika, kupitia mfumo wa TAUSI leseni 125,621 zimetolewa kwa wajasiriamali ambapo usajili huo umewezesha mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri yenye thamani ya sh. bilioni 33.4 zilizotolewa kwa vikundi 3,776 vya wanawake, vijana na wenye ulemavu.
“Kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara kwa ushirikiano na Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) wajasiriamali 16,325 (wanawake 8,462 na wanaume 7,863) wamerasimishwa.
“Wajasiriamali 11,000 wamepatiwa mafunzo ya ujasiriamali na ujuzi wa biashara, wajasiriamali 12,325 walipata mikopo kwa ajili ya kukuza mitaji yao na wajasiriamali wadogo zaidi ya 3,900 walipata namba za mlipa kodi (TIN) na leseni za biashara.
“Hivyo, hatua hizo zimechangia kuongezeka kwa kiwango cha urasimishaji, kuimarisha ajira binafsi, ajira ndogo, kuweka msingi imara wa ukuaji biashara ndogo na kukuza mchango wake katika uchumi wa Taifa.
Alibainisha: “Pia, kupitia TBS mafunzo ya uzalishaji bidhaa kwa ubora na usimamizi wa biashara ni 1,059 na bidhaa za wajasiriamali 192 zilipewa nembo ya ubora kisha kuingia sokoni kwa ajili ya ushindani.”
Waziri huyo alisema huduma ya mikopo iliyotolewa kupitia SIDO kwa wajasiriamali wadogo kuanzia Novemba mosi mwaka jana hadi kufikia Januari 23 mwaka huu, mikopo 265 yenye thamani ya sh. bilioni moja ilitolewa.
FURSA SEKTA YA UVUVI
Kwa mujibu wa Dk. Gwajima, wajasiriamali 4,578 wanaohusika katika masuala ya uvuvi, walirasimishwa ambapo kati yao vavuvi ni 2,100 na wafugaji viumbe maji ni 2,478.
Pia, alibainisha kuwa, vyama vya ushirika vya mifugo vilivyorasimishwa ni 126 na mashamba ya mifugo yaliyotembelewa na kujengewa uwezo ikiwemo kupatiwa huduma za chanjo za mifugo ni 173,147.
“Vijana 317 wamerasimishwa na kuwezeshwa kuwekeza katika miradi ya ufugaji samaki kwenye vizimba (vijana 164) na uwekezaji kwenye ufugaji majongoo bahari, kilimo cha mwani na unenepeshaji kaa.
Aliongeza: “Serikali imetoa sh. bilioni saba kuwezesha utekelezaji wa miradi hiyo.”
Kadhalika, serikali kupitia Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA), imetoa mafunzo ya ufugaji samaki kwenye vizimba kwa vijana 150, usindikaji na biashara kwa wanawake 200 ambao ni wajasiriamali kutoka mkoani Mwanza.
Alisema kupitia mpango wa kuwafikia na kuwaelimisha wajasiriamali, wadau wanaohusika na masuala ya mifugo, wanufaika 8,024 waliwezeshwa kisha kurasimishwa.
Katika kusambaza teknolojia ya kisasa ya ufugaji, alisema mbuzi wa mbegu 177 walioboreshwa wamesambazwa kwa wanufaika mbalimbali nchini katika mikoa ya Dodoma, Mwanza na Kilimanjaro huku ng’ombe wa mbegu 45 wamesambazwa Dodoma, Iringa na Pwani.
“Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) vijana 282 (wanawake 80 na wanaume 202) wamerasimishwa kisha kuwezeshwa kufanya kilimobiashara katika eneo la shamba lililotengwa lenye jumla ya ekari 6,465.69, Kaliua mkoani Tabora.
Pia, alibainisha kuwa wakulima 532,023 wamesajiliwa na kurasimishwa katika mfumo wa ruzuku ya mbolea.
MIKOPO SEKTA YA MADINI
Vilevile, alisema serikali kupitia Wizara ya Madini imerasimisha wachimbaji wadogo 2,239 kisha kuwawezesha kufanya shughuli zao za uchimbaji na kupata fursa za mikopo kutoka katika taasisi za kifedha kwa ajili ya kukuza mitaji ya shuguli wanazofanya.
Waziri Gwajima, alisema serikali katika kuhakikisha kuwa wafanyabiashara ndogondogo na wajasiriamali wanapata masoko ya uhakika, Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), imerasimisha vikundi 1,216 vya makundi maalum ya wanawake, vijana, wenye ulemavu na wazee katika Mfumo wa Ununuzi wa Umma (NeST).
“Hatua hii inawawezesha wafanyabiashara ndogondogo kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya manunuzi ya umma yaliyotengwa kwa makundi maalumu.
“Jumla ya vikundi 1,123 vimepata zabuni za ununuzi katika miradi ambapo vikundi vya wanawake 426 vilipata zabuni zenye thamani ya sh. bilioni 13.7, vikundi vya vijana 630 vilipata zabuni zenye thamani ya sh. bilioni 15.4.
Aliainisha: “Vikundi vya watu wenye ulemavu 25 vilipata zabuni zenye thamani ya sh. milioni 233.2 na vikundi vya wazee 42 vilipata zabuni zenye thamani ya sh. bilioni 1.7.”
Katika kurasimisha na kuwezesha wajasiriamali nchini, alisema serikali inashirikiana na taasisi za kifedha kutoa mikopo kwa wajasirimali kupitia taasisi hizo.




