Na AMINA KASHEBA
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amemtaka Msajili wa Vyama vya Michezo nchini, Abel Ngilangwa kuhakikisha anawapatia majibu uongozi wa klabu ya Simba juu ya mchakato wao wa mabadiliko ya katiba.
Makonda alitoa kauli hiyo Dar es Salaam katika tukio la utiaji saini mkataba wa kocha wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, Miguel Gamondi.
“Msajili wa vyama unatakiwa kuwapatia majibu uongozi wa Simba ndani ya mwezi huu wawe wameshapatiwa majibu na kuendelea na shughuli zao, kuleta maendeleo ya mchezo nchini.
“Unatakiwa kutumia mfumo wa kanuni na sheria kwa lengo la kuwapatia majibu Simba ili waendelee na shughuli zao, nakupa mwezi moja wawe wamepata muafaka wao maana wewe ndiyo msajili wa vyama vya michezo,” alisema.
Alisema Simba wanatakiwa kupatiwa majibu yao ili waendelea na mchakato wao wa mabadiliko, kuliko kukaa kimya bila kupatiwa majibu kutoka ofisi ya msajili wa vyama vya michezo.
Gazeti hili, Msajili wa Vyama Vya Michezo, Ngilangwa alieleza kwamba walipokea katiba kutoka Simba na wanaendelea kuchakata kwa lengo la kupata majibu mazuri ambayo watayatoa.
“Tumepokea katiba kutoka Simba hivi sasa tupo katika mchakato, majibu yatatoka mwezi huu kama Waziri, Makonda alivyotupa maelekezo kwani bado tunaendelea kufanyia kazi,” alisema.
Msajili huyo alisema baada ya kukamilisha kazi hiyo, wataitisha mkutano na waandishi wa habari ili kutoa majibu juu ya jambo hilo la Simba.
Wakati huo huo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amezipongeza timu za Yanga, Simba, Azam FC na Singida Black Stars zilizokuwa zikishiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho Afrika.
Yanga na Simba zilishiriki Ligi ya Mabingwa Afrika wakati Azam na Singida Black Stars walikuwa Kombe la Shirikisho Afrika na kuishia hatua ya makundi ya michuano hiyo.
Makonda akizungumza Dar es Salaam, jana, alisema ni mara ya kwanza Tanzania inafanikiwa kuingiza timu nne katika hatua ya makundi katika michuano hiyo mikubwa.
“Pongezi kwa uongozi wa timu zote, kwani mmefanya kazi kubwa ya kuhakikisha wachezaji wanapambana na kufika mbali, lakini mpira unakuwa na matokeo yake ndani ya dakika 90 za mchezo,” alisema.
Waziri huyo aliongeza kuwa ana imani timu hizo, zimefunza na kupata elimu ambayo wataitumia katika michuano ya msimu ujao na kupeperusha vyema bendera ya taifa na kuiletea sifa nchi.
“Najua mmepata somo na mmejifunza vizuri,nina imani michuano ya msimu ujao mtajipanga vyema na kupeperusha vizuri bendera ya taifa,” alisema.




