Na ATHNATH MKIRAMWENI, Urambo
MRADI mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda mkoani Tabora, ambao ni sehemu ya Gridi ya Taifa ya Maji, uko katika hatua za mwisho kukamilika.
Mradi huo, unatajwa kuwa suluhisho la kudumu la changamoto ya maji katika Wilaya za Urambo, Kaliua na Sikonge.
Mradi huo, wenye lengo la kuunganisha mikoa ya kanda za magharibi na chanzo kikuu cha maji Ziwa Victoria, unagharimu zaidi ya sh. bilioni 143, ukijumuisha ujenzi wa tanki lenye uwezo wa kuhifadhi lita milioni mbili na mtandao mkubwa wa mabomba.
Pia, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeagiza mradi huo, ukamilike ndani ya siku 14 ili kila mwananchi anufaike.
Akizungumza wilayani Urambo katika ziara yake ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Katibu wa NEC ya CCM, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi za Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2020–2025, kuhakikisha upatikanaji wa maji, unafikia asilimia 95 mijini na asilimia 85 vijijini.
Kihongosi, alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan, kutoa fedha za kutosha kuhakikisha mradi huo unatekelezwa na maji yanasafirishwa kutoka Ziwa Victoria hadi Urambo kupitia Gridi ya Taifa ya Maji.
Alisema Urambo ilikuwa na changamoto kubwa ya maji muda mrefu, hivi sasa wananchi wana kila sababu ya kuipongeza serikali kwa hatua hiyo kubwa ya maendeleo.
Kwa mujibu wa wataalamu, majaribio ya maji yanatarajiwa kuanza ndani ya wiki mbili kufuatia maagizo ya Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, huku sh. milioni 500, zikitolewa kununua mabomba ya kuunganisha mfumo mpya na ule wa zamani ili huduma ianze mapema.
Kihongosi, aliipongeza wizara husika, wataalamu wa mkoa, wilaya na wakandarasi kusimamia mradi huo kwa ubora, akisema kazi iliyofanyika inaonekana ya viwango.
Alitoa rai kwa wataalamu, kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na wananchi wanaanza kupata maji, akisisitiza watu hawahitaji kuona mabomba na matanki pekee, bali wanahitaji huduma.
Pia, aliagiza maeneo yanayozunguka tanki la maji, yahakikishiwe yanapatiwa vituo vya kuchotea maji, ili wakazi wa karibu wasiachwe nyuma maji yakisambazwa maeneo mengine.
Kihongosi, alisema kukamilika mradi huo kupitia Gridi ya Taifa ya Maji, ni mwanzo wa sura mpya ya maendeleo katika Wilaya ya Urambo na Mkoa wa Tabora.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji ya Usafi wa Mazingira Tabora, Mhandisi Mayunga Kashilimu, alisema mradi huo, utakuwa na faida kubwa kwa wakazi wa Wilaya za Sikonge, Urambo na Kaliua.
Mbunge wa Jimbo la Urambo, Margareth Sitta alimshukuru Rais Dk. Samia kuielekeza serikali kupelekea mradi huo ambao utakuwa suluhisho la muda mrefu kwa changamoto ya maji katika jimbo hilo.




