Na NASRA KITANA, Kahama
KOCHA wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Miguel Gamondi amewaomba Watanzania na wadau wa soka kutokuwa na wasiwasi na timu yao, kwani amejipanga kuboresha zaidi kikosi hicho kabla ya michuano ya Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
Tanzania itakuwa mwenyeji wa mashindano hayo yanayotarajiwa kuanza mwezi Julai, mwakani ikishirikiana na nchi za Kenya na Uganda.
Akizungumza Kahama mkoani Shinyanga baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, Gamondi alisema Watanzania wote wana matumaini kibao na kikosi chake, hivyo aliwatoa hofu kuwa wataenda kufanya vizuri.
“Niwaambie tu wadau wa soka nchini, hawatakiwa kuwa na hofu kwani nataka kufanya kazi ya kujenga kikosi imara ili kifanye vizuri katika michuano ya AFCON 2027,” alisema.
Hata hivyo, Gamondi alisema anahitaji kufanya kazi ya maandalizi ya mapema kuelekea katika mashindano hayo, lengo ni kuona wapi kuna upungufu.
Kocha huyo alisema kwamba anahitaji mechi nyingi za kirafiki ili kikosi chake kipate uzefu zaidi kabla ya kuanza mashindano hayo.
Aliongeza kuwa anajivunia kuwa na wachezaji wengi vijana ambao watajenga kikosi kizuri.
Aidha, baadhi ya wajumbe wa mkutano mkuu wa TFF, wamewashauri wachezaji watakaoitwa katika kikosi waweka mbele uzalendo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wajumbe hao, ambao waliudhuria mkutano mkuu wa 20 wa TFF uliofanyika Kahama, Shinyanga walisema wana imani timu hiyo itafanya vizuri.
Mjumbe wa kamati ya Utendaji ya Yanga, Alex Ngai alisema anapenda kuwashauri wachezaji wa Taifa Stars hasa kuelekea katika michuano ya AFCON wahakikishe wanaongeza juhudi na kujituma zaidi.
“Kuwa wenyeji wa AFCON ni heshima kubwa kwetu, hivyo wachezaji wa timu yetu wanatakiwa kuwa watulivu, kujituma na kuonyesha nia ya dhati ya kupambana ili tuweze kutwaa taji hilo,” alisema Ngai.
Mjumbe wa kamati ya utendaji TFF, Lameck Nyambaya alisema kwamba wana imani kubwa na timu yao ya Taifa hivyo wachezaji wanatakiwa kupambana kwa jasho na damu ili kufanya vizuri na kupata matokeo chanya.
“Mimi sina wasiwasi na timu yetu ya Taifa, kwani tunahitaji kuona tunapata matokeo mazuri katika mashindano hayo, hivyo wachezaji wetu wanatakiwa kushirikiana ili kufanya vizuri,” alisema Nyambaya.
Naye mjumbe wa Mkutano mkuu, Murtaza Mangungu alisema imani yake ipo kwa wachezaji wa Stars hivyo wanatakiwa kuongeza nguvu zaidi ili kuwapa furaha Watanzania.
“Tunaingia katika mshindano hayo tukiwa tuna uhakika wa kufanya vizuri katika mashindano hayo, lakini wachezaji wetu wanatakiwa kujua umuhimu wa kupambana na kurekebisha upungufu wote tufanye vizuri,” alisema Mangungu.
Mashindano hayo yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi mwezi Julai, mwakani huku wenyeji wakiwa ni Tanzania, Kenya na Uganda.




