Na ABDUL DUNIA, Zanzibar
UNAWEZA kusema imeisha hiyo , baada ya timu za Yanga na Simba kutoka suluhu katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Pambano hilo, lilipigwa katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar ambapo timu hizo zilionesha mpira wa kiwango kikubwa huku zikikosa mabao ya wazi.
Kufuatia matokeo hayo, Yanga inaendelea kuongoza ligi hiyo, tayari imecheza mechi 11, ina pointi 29 wakati Simba imefikisha alama 24 baada ya kushuka dimbani mara 11, ikiwa nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga imeshinda mechi tisa na kutoka sare mara mbili, ikifunga mabao 27 na kuruhusu mawili huku Simba ikishinda mechi saba, sare imepata katika michezo mitatu na imefungwa mechi moja.
Simba imepachika mabao 18 na kuruhusu mabao manne kutinga katika nyavu zao.
Hata hivyo, Wekundu wa Msimbazi walikuwa na nafasi kubwa ya kufuta uteja mbele ya Yanga katika pambano hilo, kama wangetumia vizuri nafasi walizopata za kupachika mabao.
Lakini wachezaji wa Simba walipoteza nafasi nyingi za kufunga mabao, walipoteza nafasi hizo na kusababisha timu hizo kutoka suluhu.
Simba ilitawala kwa kiasi kikubwa kipindi cha kwanza ikiwalazimisha Yanga kufanya makosa mara kwa mara.
Timu hiyo, ilipata nafasi nyingi kipindi cha kwanza lakini ukosefu wa umakini wa ‘mastraika’ wake na ubora wa kipa Djigui Diarra alikua kikwazo kuandika bao la kuongoza.

Miongoni mwa nafasi ilizozipata Simba katika kipindi cha kwanza ni ya Inno Loemba ambaye alipiga shuti lakini Diarra akaokoa.
Pia, Anicet Oura ambaye alikosa bao baada ya kupiga shuti kwa mguu wa kulia lakini Diarra aliokoa kwa kupangua mpira.
Kipindi cha pili, kilianza kwa kasi ambapo Prince Dube alikosa bao la wazi baada ya kutokea piga nikupige katika lango la Simba na kufumua shuti lililodakwa na kipa wa Simba, Kassali.
Dakika ya 69, Inno Loemba wa Simba alipiga shuti ambalo lilipaa juu ya lango la Yanga.
Katika dakika ya 79, Simba ilipata bao lakini mwamuzi wa pembeni alikataa bao hilo.
Selemani Mwalimu alipiga mpira huo kwa kichwa uliokwenda wavuni, lakini mshika kibendera, Kassim Mpanga alionesha ishara kwamba mchezaji huyo kabla ya kufunga alikuwa ameotea.
Dakika kadhaa baadae, De Reuck alipiga mpira kwa kichwa lakini uligonga mwamba.
Katika dadika za nyongeza, Ellie Mpanzu alipata nafasi, lakini alipiga shuti lake la mguu wa kulia, liliokolewa na Diarra.
Awali, Yanga ilikuwa ya kwanza kuwasili uwanjani saa 12:15 jioni wakati Simba ikiingia uwanjani saa 12:35 jioni kwa ajili ya pambano hilo.
Katika mpambano huo, Dickson Job aliumia na nafasi yake ilichukuliwa na Bakari Mwamnyeto.
Pia, Damaro wa Yanga alipewa kadi ya njano na mwamuzi, Nassoro Mwinchui kutoka Tanga, baada ya kumfanyia madhambi mchezaji moja wa Simba.
Baada ya mchezo huo, kipa Diarra alitangazwa mchezaji bora wa mechi kufuatia kuokoa hatari mbalimbali langoni.
Hata hivyo, Mwamnyeto baada ya mchezo huo alikiri mchezo huo ulikuwa mgumu kwa upande wao na wanashukuru kupata alama moja mbele ya watani wao wa jadi.

Clatous Chama alisema wanashukuru kumaliza salama mchezo huo na kupata pointi moja huku akieleza kuwa wana imani wanaendelea kupambana ili msimu huu waweze kutwaa ubingwa wa ligi kuu.
Yanga: Djigui Diarra, Israel Mwenda, Mohamed Hussein, Dickson Job/Bakari Mwamnyeto, Ibrahim Bacca, Damaro, Maxi Nzengeli, Duke Abuya, Depu, Mudathir Yahya/Allan Okello na Prince Dube.
Simba: Kassali, Shomari Kapombe, Nickson Kibabage, Toure, Toure, De Reuck, Yusuph Kagoma, Libasse Gueye/ Elly Mpanzu, Kante/Seleman Mwalimu , Anicet Oura, Inno Loemba na Clatous Chama.




