Na ZIANA BAKARI
MAKAMU wa Rais, Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema ifikapo mwaka 2050 Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF) yanapaswa kubadilika kutoka kuwa eneo la kuonyesha bidhaa pekee na kuwa kitovu cha ubunifu, utafiti, teknolojia pamoja na biashara za kimataifa.
Akizungumza katika hafla ya utoaji wa tuzo kwa washiriki na wadau wa maonesho hayo, Dk. Nchimbi amesema kufanikisha maono hayo kunahitaji kuendelea kuimarisha sekta ya viwanda na uzalishaji nchini, huku upatikanaji wa mitaji ukipewa kipaumbele.
Amesema mitaji ni nguzo muhimu katika kukuza uwekezaji, kuongeza uzalishaji na kuwezesha viwanda kuzalisha bidhaa zenye ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
Aidha, amewataka washindi wa tuzo hizo kutoridhika na mafanikio waliyoyapata, bali waendelee kuboresha bidhaa na huduma zao, kuongeza uzalishaji na kuchangia kwa kiwango kikubwa zaidi ukuaji wa uchumi wa taifa.
Dk. Nchimbi amesema Serikali inatarajia tuzo hizo ziwe chachu ya ubunifu, ushindani, uwekezaji na uzalishaji wenye tija, ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na maendeleo ya viwanda katika ukanda na kimataifa.




