Na IRENE MWASOMOLA
HALMASHAURI Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), chini ya Mwenyekiti wake Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imempendekeza Deogratius Ndejembi (43), kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Uamuzi huo ulitangazwa na Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Asha Rose-Migiro, katika ofisi ndogo za Chama hicho, Lumumba jijini Dar es Salaam.
Dk. Migiro alisema uamuzi wa Ndejembi kuwa Makamu wa Rais, utafanyika baada ya utaratibu wa kikatiba kukamilika.
“Uamuzi muhimu uliofanywa na Halmashaurui Kuu, ni kupokea na kupitisha jina katika hatua ya awali la mtu ambaye atapendekezwa kwa mujibu wa taratibu za Katiba kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na huyo ni Deogratius Ndejembi,”alisema Dk. Migiro.
Dk. Migiro alisema baada ya kupendekezwa jina hilo, litapelewa bungeni jijini Dodoma na taratibu za kumuapisha zitaanza.
Ndejembi ambaye ni Waziri wa Nishati, anachukua nafasi ya Dk. Emmanuel Nchimbi, ambaye alitangaza kujiuzulu Agosti 25, mwaka huu.
Nchimbi afutwa uanachama
Aidha, Dk. Migiro alisema CCM imemfuta uanachama Dk. Nchimbi kwa kukiuka katiba na kanuni za CCM.
Alifafanua Dk. Nchimbi, alikuwa akikabiliwa na makosa ya nidhamu na maadili.
“Leo tarehe 26 vilifanyika vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM, vilikuwa na ajenda za jumla ambazo zilijadiliwa, kati ya ajenda zilizojadiliwa kulikuwa na suala la nidhamu na maadili, ambalo lilikuwa linamkabili mwanachama mwandamizi wa Chama chetu, Mjumbe wa Kamati Kuu na Halmshauri Kuu Balozi Emmanuel Nchimbi.
“Vikao vyote vilijadili kwa makini masuala yaliyohusu nidhamu na maadili, na baada ya kuzingatia taarifa zote zilizokuwepo ilithibitika kwamba Katiba ya CCM pamoja na kanuni zake zilikiukwa, kufuatia hayo Halmashauri Kuu ilipitisha uamuzi kutokana na mwenendo uliokiukwa ndugu Nchimbi afukuzwe uanachama,”alisema Dk. Migiro.




