Na MWANDISHI WETU
TUME ya Madini nchini imeanza kuchukua hatua kali kwa wamiliki wa miradi 42 ya uchimbaji madini kupitia leseni ndogo za uchimbaji zenye mikataba ya Msaada wa Kiufundi (TSA) ambayo imebainika kutofanyakazi kwa mujibu wa sheria na kanuni.
Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni wahusika kupewa siku 30 kutoa maelezo ya kina na endapo wakishindwa kufanya hivyo, tume itachukua hatua za kisheria ikiwemo kufuta ridhaa ya msaada wa kiufundi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa leo (Agosti 26, 2026), Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amesema tume imefanya ukaguzi miradi yote ya uchimbaji mdogo wa madini yenye mikataba ya msaada wa kiufundi.
“Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, aliielekeza Tume ya Madini kufanya ukaguzi wa miradi yote ya uchimbaji madini kupitia leseni ndogo za uchimbaji wa madini zenye mikataba ya msaada wa kiufundi ili kufanya tathmini ya utekelezaji wa mikataba hiyo kwa kuzingatia Sheria ya Madini, Sura 123.
Ameongeza: “Kufuatia maelekezo hayo, Tume ya Madini imefanya ukaguzi wa miradi yote ya uchimbaji mdogo wa madini yenye mikataba ya msaada wa kiufundi ili kuhakiki utendaji kazi wa miradi hiyo, uzingatiaji wa masharti ya mikataba pamoja na matakwa ya sheria na kanuni zake kwa wamiliki wa leseni pamoja na watoa msaada wa kiufundi.”




