Na MWANDISHI WETU
ZIARA ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenan Kihongosi, mkoani Mwanza, imerejesha matumani kwa wananchi wa jiji hilo.
Kihongosi ambaye amefanya mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Furahisha, Nyamagana mkoani humo, ametatua baadhi ya changamoto za wananchi papo kwa papo.
Miongoni mwa wananchi waliotatuliwa changamoto zao ni mama mmoja aitwaye Happiness Benedict, aliyeomba msaada wa matibabu kutokana na tatizo la kusagika kwa nyonga lililomsumbua kwa takribani miaka mitano.
Amesema madaktari walimwambia anatakiwa kufanyiwa upasuaji, ambapo gharama ya matibabu inakadiriwa kufikia zaidi ya Sh. milioni 14.
Happiness amesema awali alikuwa na bima ya afya lakini ilikwisha muda wake, hivyo sasa hana uwezo wa kumudu gharama za matibabu.
“Hatuwezi kushindwa kupata Sh. milioni 14 au 15 kwa ajili ya kuokoa maisha ya mtu, tutashughulikia suala hili,” amesema Kihongosi.
Baada ya kumalizika mkutano, Kihongosi alimwita DMO kumhabarisha kuwa amepokea kiasi cha Sh. milioni 15 kupitia akaunti ya NMB kwa ajili ya matibabu ya Happiness.
Pia, amesaidia kupatikana kwa ada ya mwanafunzi wa chuo ambaye aliomba msaada katika mkutano huo ili aweze kuendelea na masomo, na fedha hizo zilipatikana hapo hapo.




