Na LILIAN JOEL, Arusha
SERIKALI imesema ukwasi wa mifuko ya hifadhi ya Jamii nchini umeongezeka kutoka sh. trilioni 10.43 Juni, mwaka 2020 hadi sh. trilioni 24.20 Desemba,mwaka jana.
Pia, serikali imelipa sh. trilioni 4.26 sawa na asilimia 95 ya deni la michango ya wanachama wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) la sh. trilioni 4.46 la kabla ya Juni, 1999 na kiasi kilichobaki, Rais Dk, Samia Suluhu Hassan, ameridhia ufanyiwe uhakiki.
Kauli hiyo, ilitolewa jijini Arusha, jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu kwa niaba ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, alipofungua mkutano mkuu wa wadau wa sekta ya kinga ya jamii.
Sangu, alisema ongezeko la ukwasi huo ni matokeo ya uboreshaji wa sera, sheria na utendaji.
Kwa mujibu wa Sangu, hivi sasa thamani ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ni sh. trilioni 10.40, PSSSF sh. trilioni 12.96 huku Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), ukiwa ni sh. bilioni 844.41.
Kuhusu uwekezaji, Sangu alisema uwekezaji wa mifuko umeongezeka kutoka sh. bilioni 9.39 Juni, 2020 hadi sh. bilioni 20.13 Desemba, mwaka jana na kiasi hicho kilitokana na ongezeko la uwekezaji wa mfuko wa NSSF kutoka sh. bilioni 3.41 Juni, 2020 hadi sh. bilioni 8.73 Desemba mwaka jana.
“Uwekezaji wa mfuko wa PSSSF uwekezaji wake kutoka shilingi bilioni 5.66 Juni, 2020 hadi shilingi bilioni 10.5 Desemba mwaka jana na mfuko WCF, kutoka shilingi bilioni 321 Juni, 2020 hadi shilingi bilioni 892.12 Desemba, mwaka jana,” alisema.
Alisema uwekezaji huo, umefanyika katika maeneo mbalimbali ikijumuisha hati fungani za serikali na kampuni binafsi,miliki ardhi, hisa katika masoko ya mitaji; amana za benki na uwekezaji wa pamoja.
“Hatua hii imeimarisha uimara wa mifuko na kuwawezesha wanachama kulipwa mafao yao kwa wakati, pensheni kulipwa tarehe 25 ya mwezi sanjari na huduma kutolewa kidijitali,”alisema.
Katika hatua nyingine, Waziri Sangu, alizindua skimu ya wananchi waliojiajiri katika sekta isiyo rasmi chini ya mfuko wa NSSF ikiwa ni mkakati wa kuwajumuisha wananchi katika mfumo wa kinga ya jamii sanjari na
Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii ya mwaka 2023, inayotoa mwelekeo wa utekelezaji wa haki ya kinga ya jamii kwa Watanzania na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050
“Hadi hivi sasa, zaidi ya wananchi 509,000 kutoka makundi ya wakulima, wafugaji, wavuvi, bodaboda na mama lishe wamejiunga, huku lengo likiwa kuwafikia zaidi ya milioni 5.5 ifikapo mwaka 2031,” alisema.
Sangu aliwataka wadau wa mifuko ya hifadhi ya jamii, kuimarisha utoaji wa huduma kwa kuhakikisha taarifa za wanachama zinakuwa sahihi na waajiri wote wanawasilisha michango kwa wakati.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mary Maganga, alisema mkutano huo ni jukwaa muhimu la wadau kujadili kwa pamoja namna bora ya kuimarisha utekelezaji wa sera, skimu na mifumo ya kinga ya jamii kwa maslahi mapana ya Watanzania.
Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Kamati ya kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), Hawa Chakoma, alisema Bunge halitakuwa kikwazo katika utekelezaji wa sera na skimu ya wananchi waliojiajiri, hususan wajasiriamali, bali litaendelea kushirikiana na serikali kuhakikisha utekelezaji wake unafanikiwa.
Mkurugenzi Mkuu WCF, Dk. John Mduma, alisema mfuko huo umekuwa mfano wa kuigwa katika utoaji wa fidia kwa wafanyakazi wanaoumia kazini, hali iliyovutia nchi mbalimbali zikiwemo Kenya, Zimbabwe, Afrika Kusini na Malawi kuja kujifunza mfumo wa uendeshaji wa huo.




