Na VICTOR MKUMBO, Zanzibar
MKONGWE wa muziki raia wa Mali, Salif Keita, juzi alishindwa kutokea katika kufunga tamasha la burudani la Kimataifa la Sauti za Busara kutokana na tatizo la kiafya.
Tamasha hilo la aina yake lilihitimishwa kwa burudani kabambe kutoka kwa wasanii mbalimbali ambapo msimu huu lilifanyikia katika Uwanja wa Mnazi Mmoja visiwani hapa.
Salif Keita mwenye mashabiki lukuki, alikuwa akisubiriwa kwa hamu kupanda jukwaani na kutoa burudani murua lakini kwa bahati mbaya hakutokea kutokana na tatizo la afya linalomkabili.
Hata hivyo bendi yake iliyosheheni wanamuziki mahiri ilitoa burudani ya aina yake bila yeye na kukonga nyoyo za mashabiki.
Katika hitimisho la tamasha la Sauti za Busara, bendi ya Keita ilikuwa ya mwisho kupanda jukwaani ambapo wasanii wake walianza kuimba kuanzia saa 6:00 usiku hadi saa 7:10 usiku na kutoa burudani iliyokata kiu ya mashabiki wake.
Katika tamasha hilo, bendi hiyo iliimba kibao cha ‘Afrika’ na kuufanya umati wa mashabiki kushangilia kwa kiasi kikubwa na kukonga nyoyo zao.
Akizungumza visiwani hapa, Mkurugenzi wa Sauti za Busara, Journey Ramadhan alisema mkongwe wa muziki Keita alishindwa kusafiri na bendi yake kutokana na tatizo la afya linalomkabili.
Alisema hadi dakika za mwisho, Keita mwenye umri wa miaka 76 alikuwa mmoja wa wasanii wakubwa watakaotyumbuiza katika tamasha hilo lakini kwa bahati mbaya daktari wake aliwapa taarifa kwamba hatahudhuria kutokana na tatizo la afya.
Hata hivyo walipanga kuiondoa bendi hiyo kutokana na Keita kupata tatizo la afya lakini mkongwe huyo alikataa na kuamua kuwatuma bendi yake kuhakikisha wanatoa burudani murua kwa mashabiki lukuki ambao walisubiri tamasha la Sauti za Busara kwa muda mrefu.
“Tulitarajia Keita atatufungia tamasha letu kwani ni mmoja wa wasanii wakubwa ambao walitakiwa kutoa burudani katika siku ya mwisho lakini ilishindikana kusafiri kutokana na tatizo la afya linalomkabili.
“Hadi dakika za mwisho wakati tunaendelea na maandalizi Keita alikuwa tayari kuja kuungana na sisi lakini baadaye daktari wake alitoa taarifa kwamba haitawezekana kuja kutokana na afya yake kutokuwa vizuri.
“Tulishauriana na Keita kwamba tuondoe katika orodha bendi yake lakini mwenyewe alikataa na kusisitiza atawatuma vijana wake ambao kila mmoja ameshuhudia burudani yao jukwaani.
“Pamoja na changamoto zilizotokea, tumeona vijana na wanawake walivyopewa nafasi na kutoa burudani murua na kila shabiki amefurahia kwani bendi imekuja na kutoa burudani ya aina yake bila yeye,” alisema mkurugenzi huyo.
Tofauti na ‘Afrika’, bendi hiyo iliimba nyimbo zingine za ‘Yamore’, ‘Tekere’, ‘Lony’, ‘Tomorrow’, ‘Yaye Boy’, ‘Mopao’, ‘Madan’ na ‘Mousoulou’ ambazo zilikonga nyoyo za mashabiki.




