ABDURAHIM MZAKILU, JENIPHER MWACHIPA (UDSM) Na NASRA KITANA
WAKATI Yanga na Simba zikishuka dimbani kesho, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limefichua kuwa, sababu ya mechi hiyo kupigwa Zanzibar ni ubora wa Uwanja wa New Amaan Complex.
Yanga na Simba zitachuana katika Ngao ya Jamii kesho saa 2:30 usiku katika Uwanja wa New Amaan, Zanzibar.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo, alisema uwanja wa New Amaan ni bora na unastahili kutumika kwa mtanange huo.
“Niseme tu hadi sasa uwanja huo upo tayari kwa mchezo wa Ngao ya Jamii baada ya kuufanyia ukaguzi na kujiridhisha kwa asilimia kubwa ubora wake,” alisema Ndimbo.
Hata hivyo, Ndimbo alisema kuwa wanatarajia leo kutangaza majina ya waamuzi ambao watachezesha mchezo huo muhimu.
Wakati huo huo, Ndimbo alisema TFF imezindua mfumo mpya wa kununua tiketi ambapo kwa sasa zitapatikana kwa njia ya mtandao wa shirikisho hilo.
Ndimbo alisema mfumo huo ni rahisi kuutumia unatoa fursa ya kununua tiketi nne kwa mtu mmoja kwa kutumia tovuti ya WWW.TFF-TICKET.COM.
“Kwa sasa tiketi zote zitakazonunulia katika mfumo mpya, zitakuwa na majina, mfumo huo utaanza kutumika rasmi leo (jana), lengo ni kuboresha mpira wetu na kuwa Kidigital,” alisema Ndimbo.
Timu hizo zimekutana katika fainali hiyo baada ya Yanga kuwa mabingwa wa Ligi Kuu msimu wa 2025/26 huku Simba ikiwa bingwa wa Kombe la FA.



