Na MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameridhia kujiuzulu kwa Makamu wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, kuanzia Septemba 4, mwaka huu.
Pia, Rais Dk. Samia amesema taratibu za kikatiba za kumpata Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwingine, zitachukuliwa.
Taarifa iliyotolewa kwa umma na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dk. Moses Kusiluka, ilieleza Rais Dk. Samia alipokea barua ya ombi la kujiuzulu Balozi Dk. Nchimbi.
“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dk. Samia Suluhu Hassan, leo (jana), amepokea barua ya ombi la kujiuzulu Makamu wa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, kuanzia tarehe 04 Septemba, 2026. Mheshimiwa Rais ameridhia ombi hilo, taratibu za kikatiba za kumpata Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwingine zitachukuliwa,” ilieleza taarifa hiyo ya Katibu Mkuu Kiongozi.
BARUA YA NCHIMBI KWA RAIS
Balozi Dk. Nchimbi (55) jana alitangaza kujiuzulu ifikapo Septemba 4, mwaka huu.
Katika taarifa yake kwa umma, alieleza amemwandikia barua Rais Dk. Samia kumjulisha uamuzi wake huo.
“Agosti 25, 2026, nimemwandikia barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, kumjulisha kuwa, nimeamua kustaafu siasa na utumishi wa umma.
“Hivyo nitajiuzulu nafasi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuzingatia ibara ya 50 (2) (c), ikisomwa kwa pamoja na ibara ya 149 (2) ya katiba kuanzia Septemba 4 mwaka huu,” ilieleza taarifa hiyo.
Katika taarifa yake hiyo, Dk. Nchimbi aliandika Agosti 27 mwaka jana, alimwahidi Rais Dk. Samia kuwa, atamsaidia yeye na nchi kwa uwezo wake wote na kwa uaminifu.
Kupitia taarifa hiyo, Dk. Nchimbi alieleza alimhakikishia Rais Dk. Samia siku yoyote akiona anahitaji Makamu wa Rais mwingine, ataachia nafasi hiyo.
“Nimejiridhisha pasipo na shaka, Rais anatamani mabadiliko, hivyo nimeamua kutimiza ahadi yangu.
“Kipekee namshukuru Rais na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa imani yao kwangu, natumia nafasi hii pia kuwashukuru Watanzania wote kwa ushirikiano mkubwa mlionipa wakati wote niliokuwa katika utumishi wa umma nawahakikishia nitaendele kuwa raia mwema wa Tanzania, “ ilieleza taarifa hiyo ya Dk. Nchimbi.
KATIBA INAVYOTAMKA
Ibara ya 50 – (2) (C) inaeleza kwamba, Makamu wa Rais atashika kiti hicho hadi…
(a) Muda wake utakapokwisha;
(b) Akifariki dunia akiwa madarakani;
(c) Atakapojiuzulu;
Ibara ya 149 (2) inaeleza;
Mtu aliyetoa taarifa ya kujiuzulu kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (1) ya ibara hii, atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku ile ambayo taarifa yake ya kujiuzulu itakapopokewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika au itakapopokewa na mtu yeyote aliyeruhusiwa kuipokea taarifa hiyo na mtu anayehusika au kikao kinachohusika, lakini kama taarifa hiyo ya kujiuzulu imeeleza kwamba mtu huyo atajiuzulu tangu siku nyingine baada ya taarifa hiyo kupokewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika, basi mtu huyo atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku hiyo nyingine ya baadaye.
MGOMBEA MWENZA
Januari19, mwaka jana, Mwenyekiti wa CCM, Rais Dk. Samia alimtangaza aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dk. Nchimbi, kuwa mgombea mwenza wake wa urais katika uchaguzi mkuu 2025.
Balozi Nchimbi, alitangazwa kwenye Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM, uliofanyika Dodoma, baada ya aliyekuwa Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango, kumwandikia barua ya kuomba apumzike na Rais Samia kuridhia ombi hilo.
Novemba 3, mwaka jana, Rais Dk. Samia na Makamu wa Rais, Balozi Dk. Nchimbi, waliapishwa jijini Dodoma, baada ya kushinda kwa asilimia 97.66 kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 29, mwaka jana.
WASIFU WA DK. NCHIMBI
Historia ya uongozi wa Dk. Emmanuel Nchimbi, inaeleza aliwahi kuwa waziri, naibu waziri kwa nyakati tofauti na katika wizara mbalimbali; amekuwa mbunge, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), balozi na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) na mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kwa nyakati tofauti.
Alikuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo mwaka 2006, Naibu Waziari wa Kaazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana 2006 hadi 2008.
Mwaka 2008 hadi 2010, alikuwa Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo 2010 hadi 2012, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi 2012 hadi 2013.
Balozi wa Tanzania nchini Brazil mwaka 2016 hadi 2021, Balozi wa Tanzania nchini Misri mwaka 2022 hadi 2023.
Mbali na nyadhifa hizo, Balozi Dk. Nchimbi ameshika nafasi mbalimbali ndani ya Chama Cha Mapinduzi, alikuwa Katibu Mkuu wa CCM mwaka 2024, mwaka 1998 alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa UVCCM. Mwaka 2005 hadi 2015 alichaguliwa kuwa mbunge wa Songea Mjini.




