Na MWANDISHI WETU, Dodoma
NAIBU Katibu Mtendaji wa Menejimenti ya Utendaji na Tathmini Tume ya Taifa ya Mipango, Sosthenes Kewe, amesema ni umuhimu kwa miradi ya umwagiliaji kuwa na matokeo yanayoonekana kwa jamii na kuzingatia vipaumbele vya taifa.
Kewe alisema hayo katika kikao baina ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) na Tume ya Taifa ya Mipango.
Kikao hicho kililenga kujadili namna bora ya kuoanisha mipango, miradi na utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa nia ya kuongeza tija kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Alieleza ni muhimu taasisi zote kuhakikisha miradi yao inaendana na mipango ya maendeleo ya muda mfupi na mrefu, huku ikionesha uwajibikaji na kuinua uchumi wa wananchi
“Tunapaswa kuzingatia miradi yenye matokeo zaidi kwa jamii, inayotanguliza vipaumbele vya taifa na kuonesha matokeo halisi yanayoboresha maisha ya Watanzania,” alisisitiza.
Alisema, sekta ya umwagiliaji ni kubwa kufikia malengo ya maendeleo ya kitaifa hivyo ni muhimu kazi zinazotekelezwa na NIRC na uwekezaji unaoenelea uendane na mipango ya nchi kwa kuzingatia malengo ya kiuchumi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Raymond Mndolwa, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na uratibu madhubuti kati ya taasisi hizo ili kuhakikisha miradi inayotekelezwa inaleta matokeo chanya.
“Ni muhimu tuanze pamoja ili kuhakikisha yale tunayoyafanya yanaendana na mipango ya nchi. Pale tunapokwenda vizuri tuendelee, lakini pia turekebishane mapema ili kuepuka upotevu wa rasilimali za serikali na kuongeza ufanisi katika utekelezaji,” alisema.
Kikao hicho pia kililenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu utekelezaji wa mipango ya maendeleo, ikiwemo uingizaji wa miradi kwenye mifumo rasmi ya ufuatiliaji na tathmini, kuongeza ubora wa taarifa za utekelezaji na kuhakikisha upatikanaji wa takwimu sahihi zitakazosaidia kuvutia uwekezaji na kuonesha mchango wa sekta ya umwagiliaji katika ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, majadiliano hayo yanathibitisha dhamira ya serikali ya kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi zake, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa ufanisi zaidi kuleta matokeo chanya, ya kudumu kwa jamii na kukuza uchumi wa nchi.



