Na IRENE MWASOMOLA
KATIBU Mkuu Kiongozi, Balozi Dk. Moses Kusiluka, amewata Maofisa Habari wa Serikali, kutumia vizuri teknolojia ya habari na kutoa ufafanuzi kwa wakati pindi zinapotokea taarifa za upotoshaji.
Amesema teknolojia ya habari imebadilika kwa kasi kubwa, hivyo inaweza kutumiwa na maadui kuhatarisha usalama wa nchi kama haitatumiwa vizuri.
Balozi Dk. Kusiluka aliyasema hayo jijini Dar es Salaam, alipofungua mkutano wa kikao kazi cha Kitaifa cha Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais na Maofisa Habari wa Serikali.
“Nilazima Maofisa Habari kuhakikisha mnajipanga vizuri kuitumia teknolojia ya habari, ili kuleta maendeleo ya nchi,” alifafanua na kuhoji:
“Sisi ni jeshi la Serikali, inakuwaje wakati mwingine tushambuliwa wakati sisi (Maofisa Habari) tumekaa?”
Alisema ni matarajio ya serikali kuona Maofisa Habari watajipanga vizuri katika kukabiliana na matumizi hasi ya teknolojia ya habari.
Aidha Balozi Dk. Kusiluka aliwaagiza Maofisa Habari kuhakikisha wanakua na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupitia utekelezaji wake ndani ya taasisi zao na kutoa taarifa kwa umma.
Vilevile aliwataka wahakikishe wanakuwa washauri wazuri kwa viongozi wao katika utekelezaji wa mikakati ya taasisi zao.
Pia, Balozi Dk. Kusiluka aliwataka Maofisa Habari kuendelea kuzingatia miiko na maadili ya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao.
MSIGWA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Gerson Msigwa alisema, kikao kazi hicho kinafanyika kwa siku mbili kuanzia jana hadi leo kitasaidia kukumbushana na kuongeza maarifa kwa Maofisa Habari.
Alisema kikao kazi hicho kimehudhuliwa na Maofisa Habari wa Serikali, Taasisi za Umma na vyombo vya usalama zaidi ya 500.
TIDO
Mshauri wa Rais Habari na Mawasiliano, Tido Mhando, alisema ni dhamira ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuona Maofisa Habari wanatoa taarifa sahihi na kwa uzalendo.
Alisema Serikali katika kuhakikisha inaboresha sekta ya habari, Rais Dk. Samia alianzisha Tume ya Kuangalia maslahi ya Vyombo vya Habari, Bodi ya Ithibati na kufanya uteuzi wa Mshauri wa Rais Habari na Mawasiliano.
Aidha Mhando alisema ni matarajio yake kwamba, Maofisa Habari wataendelea kuwa daraja zuri kati ya serikali na wananchi na kumsaidia Rais Dk. Samia.
MACHUMU
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Bakari Machumu, alisema Maofisa Habari wa Serikali na taasisi za umma ni daraja la heshima kati ya Serikali na wananchi, wakiongozwa na utu na 4R. Alisema kikao kazi hicho kinachoendelea kufanyika leo kinatumika kuwakumbusha Maofisa Habari wa Serikali wajibu wao wa kujifunza na kutumia wingi wao kama mtaji wa taifa katika kutoa taarifa sahihi na kwa wakati.




