Na NASRA KITANA
BEKI wa timu ya Taifa Stars, Shomari Kapombe amewataka wachezaji vijana kuonyesha uwezo mkubwa katika mashindano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2025), kuhakikisha wanaonekana na kupata fursa ya kusajiliwa na timu za nje ya nchi.
Stars ipo kambini nchini Misri kwa ajili ya maandalizi ya mashindano ya AFCON 2025 zinazotarajiwa kuanza Desemba 21 hadi Januari 18, mwaka huu nchini Morocco.
Tanzania ipo kundi C na timu za Uganda, Nigeria na Tunisia.
Akizungumza kuelekea katika mashindano hayo, Kapombe alisema ni fursa pekee kwa vijana kuonekana kuhakikisha wanaonyesha kiwango cha hali ya juu ili kupata fursa ya kusajiliwa timu mbalimbali.
Alisema mashindano hayo yanafuatiliwa na mawakala mbalimbali duniani na kwamba kama wachezaji vijana wakionyesha kiwango bora watapata faida ya kusajiliwa katika timu kubwa.
“Haya ni mashindano makubwa, kwa wachezaji vijana hii ni nafasi ya kuweza na kuonekana, hivyo wanatakiwa kuonyesha juhudi na kujituma ili kupata fursa ya kusajiliwa na timu mbalimbali zikiwemo za nje ya nchi,” alisema Kapombe.
Hata hivyo Kapombe alisema hiyo itakuwa ni AFCON yake ya kwanza kushiriki kwani zile zilizopita alikuwa majeruhi, ana imani atakuwa na masaada mkubwa katika timu yake.
“Tunaendelea na maandalizi mazuri kwani kila mchezaji yupo katika hali nzuri kuhakikisha tunafanya vyema katika mashindano hayo makubwa na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania,” alisema Kapombe.
Beki huyo alisema ana imani kubwa na Kocha Miguel Gamondi kuwa atawapa mbinu mbadala ya kuweza kuwakabili wapinzani wao.
Naye mchezaji wa Stars, Zuberi Foba alisema wanaendelea na maandalizi kuelekea katika mashindano hayo na ana imani watafanya vyema.
Alisema wana nia na utayari wa kuhakikisha wanapambana mwanzo hadi mwisho ili kufikia malengo waliyojiwekea.
“Tunajua haya ni mashindano makubwa na yenye ushindani, kila timu ambayo inashiriki ni bora na hivyo tutapambana kwa kila namna kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea,” alisema.
Kwa upande mwingine, Kocha Gamondi amemwongeza mshambuliaji Selemani Mwalimu wa Simba katika kikosi cha Stars kuchukua nafasi ya Abdul Suleiman ‘Sopu aliyepata majeraha mazoezini.
Wakati huo huo, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeweka wazi kuwa katika kila mechi watanunua tiketi 90 kwa ajili ya mashabiki waliopo nchini Morocco.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo, shirikisho hilo limechua hatua hiyo ili kuwawezesha mashabiki wengi kuingia uwanjani na kuisapoti Stars.
Hii ni mara ya nne, Stars kufuzu fainali za AFCON ikishiriki kwa mara ya kwanza mwaka 1980 nchini Nigeria, mwaka 2019 michuano hiyo iliyofanyika nchini Misri na mwaka 2023 ilipochezwa Ivory Coast.
Taifa Stars itaanza dhidi ya Nigeria Desemba 23, mwaka huu, kisha Desemba 27 mwaka huu itapepetana na Uganda na kabla ya kumaliza hatua ya makundi dhidi ya Tunisia, Desemba 30, mwaka huu.




