Na ABDUL DUNIA
MASHINDANO ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, yanatarajiwa kufanyika Alhamisi hii hadi Januari 18, mwakani nchini Morocco.
Fainali hizo za 35 za michuano hiyo mikubwa zaidi barani Afrika, zinatarajiwa kupigwa katika majiji sita tofauti nchini Morocco.
Majiji hayo ni Casablanca, Rabat, Marrakesh, Agadir, Fez na Tangier.
Katika maeneo hayo sita, jumla ya viwanja vya soka tisa vitatumika katika michuano hiyo.
CASABLANCA
Mji huo mkubwa zaidi katika nchi hiyo na kituo kikuu cha biashara na uchumi wa taifa hilo, unatarajiwa kuwa kivutio kikubwa zaidi kwa wageni katika michuano hiyo.
Katika jiji hilo, kuna uwanja mmoja wa soka ambao utatumika katika michuano hiyo ambao ni Stade Mohammed V ambao una uwezo wa kuingiza mashabiki 45,000.
AGADIR
Katika jiji hilo, kutakuwa na uwanja mmoja ambao utatumika katika fainali hizo ambao unaitwa Adrar wenye uwezo wa kuingiza mashabiki wa soka 45,000.
FEZ
Katika jiji hilo lililopo Kaskazini mwa Morocco, uwanja utakaotumika katika fainali za AFCON ni Fez wenye uwezo wa kuingiza mashabiki wa soka 45,000.
MARRAKESH
Marrakesh ni jiji la nne kwa ukubwa nchini Morocco ambapo jiji hilo lipo magharibi mwa milima ya Atlas.
Katika jiji hilo, Uwanja wa Marrakesh ndiyo utatumika katika fainali hizo ambao utakuwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 45,000.
RABAT
Rabat ndiyo mji mkuu wa Morocco na jiji la saba kwa ukubwa nchini humo.
Katika jiji hilo, kuna viwanja vinne vya soka ambavyo vitatumika katika fainali za AFCON mwaka huu.
Viwanja hivyo ni Prince Moulay Abdellah wenye uwezo wa kuingiza mashabiki 68,700, Moulay Hassan unaoingiza mashabiki 22,000, Rabat Olympic unaoingiza mashabiki 21,000 na Al Medina unaoingiza mashabiki 18,000.
TANGIER
Tangier ni jiji lililopo Kaskazini Magharibi mwa Morocco, katika pwani ya bahari ya Mediterranean na Atlantic.
Katika jiji hilo, uwanja wa Tangier Grand ndiyo utatumika katika fainali hizo, ambapo dimba hilo lina uwezo wa kuingiza mashabiki 75,600.
MAKUNDI
Michuano hiyo inayoshirikisha timu 24, jumla ya makundi sita yamepangwa ambapo kila kundi limehusisha timu nne.
Kundi A linaundwa na mwenyeji Morocco pamoja na timu za Mali, Zambia na Comoros wakati kundi B likiwa na Misri, Afrika Kusini, Angola pamoja na Zimbabwe huku kundi C lina timu za Tanzania ‘Taifa Stars’, Nigeria, Tunisia na Uganda.
Senegal inaunda kundi D na timu za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Benin na Botswana wakati Algeria ipo kundi E na timu za Burkina Faso, Guinea ya Ikweta na Sudan huku kundi F likiwa na bingwa mtetezi Ivory Coast na timu za Cameroon, Gabon na Msumbiji.




