NA MWANDISHI WETU
WAZIRI MKUU Dk. Mwigulu Nchemba ameutaka uongozi wa Wizara ya Afya ufuatilie suala la upatikanaji wa dawa mahsusi hospitalini kuondoa dosari ndogondogo zilizopo.
Ametoa wito huo akizungumza na viongozi wa mkoa wa Lindi na viongozi wa sekta ya afya baada ya kupokea taarifa ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi inayojengwa katika eneo la Mitwero, nje kidogo ya mji wa Lindi.
Kitengo chenu cha utafiti kifanye kazi kubaini ni aina gani ya dawa zinahitajika hapa mkoani Lindi. Bohari ya Dawa ifuatilie vizuri na kuleta dawa zinazotakiwa, amesema wakati akimwagiza Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi ambaye alikuwepo katika ziara hiyo.
Amesema usipofanyika utafiti huo, Bohari ya Dawa watajikuta wanapeleka dawa nyingi mahali ambako hazihitajiki. Unaweza kujikuta unapeleka dawa nyingi za malaria huko Zanzibar wakati wao hilo tatizo hawana kabisa, amesema.
Kuna kilio cha dawa mahsusi kukosekana katika hospitali na badala yake wagonjwa wanaambiwa waende kununua kwenye viosk. Takwimu zinaonesha kuna utoshelevu wa dawa wa asilimia 80 90 lakini katika hali halisi, watu wanaambiwa wakanunue dawa nje, amesema.
Kuhusu upatikanaji wa vifaa tiba, Waziri Mkuu amesema ndani ya miaka minne na nusu, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweza kuweka mashine za CT-Scan katika mikoa yote 26 ya Tanzania Bara ikilinganishw ana mashine mbili zilizokuwepo. Pia ameweka mashine za MRI katika hospitali zote za kanda ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibingwa, amesema.
Mapema, akitoa maelezo ya ujenzi mbele ya Waziri Mkuu, Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Alexander Makala alisema ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje umefikia asilimia 85 na baadhi ya huduma zinatolewa katika hospitali hiyo.
Alisema jengo la mionzi lililogharimu sh. milioni 231 limekamilika na linatoa huduma ambapo mashine ya CT-Scan yenye thamani ya sh. bilioni 1.8 imefungwa na inafanya kazi. Majengo mengine yaliyokamilika ni la magonjwa ya dharura (EMD) kwa gharama ya sh. milioni 650, wagonjwa mahututi (ICU) kwa gharama ya sh. milioni 560 na nyumba ya watumishi kwa gharama ya sh. milioni 55.
Amesema majengo ambayo yameshapangiwa bajeti ni ya maabara, chumba cha kufulia, chumba cha kuhifadhia maiti na jengo la huduma ya mama na mtoto.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba amekagua maendeleo ya mradi wa shule mpya ya msingi ya Likongo inayojengwa kwa ushirikiano baina ya mradi wa gesi asilia (LNG) na Shirika la Maendeleao ya Petroli Tanzania (TPDC).
Shule hiyo iliyopo katika kijiji cha Likongo itakapokamilika, itagharimu sh. bilioni 1.2 ambapo kati ya fedha hizo, Serikali imechangia asilimia 26.68, kampuni ya Shell imechangia asilimia 36.66 na kampuni ya Equinor imechangia asilimia 36.66.
Akitoa maelezo ya ujenzi wa shule hiyo mbele ya Waziri Mkuu, Mhandisi Upendo Malavano alisema shule itakapokamilika, itakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 400 ikilinganishwa na wanafunzi 270 wanaosoma kwenye shule ya zamani.
Akizungumza na wakazi wa eneo hilo, Dk. Mwigulu ametoa wito kwa wakazi wa eneo hilo na Tanzania kwa ujumla kuwapeleka watoto wao shuleni kwani Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka mazingira wezeshi katika sekta ya elimu yanayowafanya watoto wa Kitanzania kupata elimu bora.
Rais Dk. Samia aliahidi ajira za walimu katika siku 100, sasa usaili umefanyika na walimu 7000 wataajiriwa na itakapofika Januari 10, 2026 walimu hawa wataripoti katika vituo vya kazi watakavyopangiwa.
Naye, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Reuben Kwagilwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia ametoa kiasi cha shilingi bilioni 114 za kushughulikia masuala ya elimu katika mkoa wa Lindi.




