Na JOE NAKAJUMO
SHIRIKA la Afya Duniani (WHO), limesema magonjwa yasiyoambukiza yanachukua nafasi ya kwanza duniani kwa kuua watu.
Miongoni mwa magonjwa yasiyoambukiza ni shinikizo la damu, kisukari, matatizo ya figo,moyo,saratani na ini.
Haya yanaua kimya kimya. Yanachochewa zaidi na ulaji usiofaa wa vyakula vyenye mafuta mengi,chumvi nyingi,sukari kupita kiasi na nishati nyingi.
Inakadiriwa kuwa watu milioni 41,hufariki kila mwaka duniani kutokana na magonjwa yasiyoambukiza,sawa na asilimia 74 ya vifo vyote. Kugharamia matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza,dunia kwa mwaka jana 2025, zilitumika zaidi ya dola za Marekani trilioni mbili kwa mwaka.
Kwa mfano,nchini Tanzania,ukibainika figo zimefeli,uchujaji damu unagharimu siyo chini ya sh.150,000 kwa kila awamu ya uchujaji na wastani wa awamu,siyo chini ya mara tatu kwa wiki.
Tanzania,Wizara ya Afya,inasema zaidi ya asilimia 34 ya vifo vinavyotokea,vinatokana na magonjwa yasiyoambukiza.Yanayoongezeka kwa kasi ni saratani,kisukari,shinikizo la damu,magonjwa ya moyo, afya ya akili,magonjwa ya figo, selimundu na baadhi ya magonjwa ya njia ya hewa.
SARATANI TANZANIA
Kwa ugonjwa wa saratani,Shirika la Afya Duniani,limetoa takwimu kwamba jumla ya wagonjwa wapya 42,000 hadi 45,000 wanapatikana kila mwaka nchini Tanzania. Saratani ziko za aina mbalimbali, zinazowakabili wanawake na wanaume.
Taarifa inasema saratani ya shingo ya kizazi inaongoza kwa asilimia 30 ya wagonjwa,ukilinganisha na asilimia 15 ya saratani ya titi. Saratani zingine ni tezi dume na utumbo mpana.
Kwa ugonjwa wa saratani, takwimu zinaonyesha watu milioni 10 wanafariki kila mwaka duniani kwa kuugua saratani za aina mbalimbali,milioni 18 hufa kwa magonjwa ya moyo,milioni nane wanakufa kwa presha na watu milioni tano hufa kutokana na magonjwa ya kisukari.
Mwezi Machi 2023, Daktari Bingwa wa magonjwa ya moyo,Hospitali ya Taifa Muhumbili,Dk. Hassan Mwamba,alikaririwa akisema utafiti ulionyesha asilimia 30 ya vifo vyote duniani vinasababishwa na matatizo ya moyo, kutokana na matumizi ya chumvi ya mezani. Wanawake wakiongoza kwa kufa zaidi. Alisema Tanzania, kila mwaka katika vizazi hai 1,000, watoto wanane huzaliwa na matatizo ya moyo.
KEMIKALI SEHEMU ZA SIRI
Meneja wa Maradhi yasiyoambukiza, Zanzibar, Dk. Omar Mohamed Suleiman, alishauri wanawake kuacha tabia ya kutumia vitu vyenye kemikali kama chumvi na tumbaku kuweka sehemu zao za siri.
Alitoa ushauri baada ya kubainika miongoni mwa sababu za kupata saratani ya shingo ya kizazi ambayo inachukua nafasi kubwa katika maradhi yasiyoambukiza Zanzibar ni matumizi ya kemikali.
Meneja huyo akizungumzia maradhi yasiyoambukiza na madhara yake, alisema, asilimia kubwa ya wanawake hutumia vitu vyenye kemikali,mbali ya tumbaku na chumvi, pia huweka shabu, asali, ndimu na nyungu.
KANSA YA SHINGO YA KIZAZI
“Matumizi ya vitu hivyo, husababisha kuathirika kiasi kikubwa viungo vya uzazi na kupata kansa ya shingo ya kizazi. Wanawake wengi wanafanya hivyo kwa kuweka kemikali sehemu zao za siri kwa lengo la kuwaridhisha wenza wao au marafiki wanapofanya tendo la ndoa, hawajui kama yapo madhara wanayoweza kuyapata,”alisema.
Dk. Suleiman alinukuu taarifa ya Wizara ya Afya Zanzibar kwamba kuanzia mwaka 2018 hadi 2024,jumla ya wanawake 32,000,walipimwa saratani ya shingo ya kizazi,kati yao 640 walipatikana na ugonjwa wa kansa ya kizazi ukiwa katika hatua mbalimbali na wanawake 141 walikuwa katika hatua mbaya.
Meneja alifafanua kwamba hali hiyo inaonesha saratani ya shingo ya kizazi ipo na miongoni mwa kichocheo chake kikubwa ni kuweka vitu katika viungo vya uzazi.
HAIFAI KUJIFUKIZA UDI
Daktari huyo mtaalamu wa magonjwa yasiyoambukiza anadokeza kwamba wapo wanawake wenye kujifukiza udi ili wanukie mwilini. Anaonya ni hatari kwa kuwa moshi wake unakuwa na kaboni ambayo huingia sehemu ya siri na kusababisha athari kubwa.
Mtaalamu wa Afya ya Uzazi, Baba, Mama na Mtoto, Dk. Oscar Mwambapa alisema mwanamke anapoweka vitu vyenye kemikali ndani ya uke wake,vinaharibu mlango wa uzazi kwa kupata mchubuko.
Dk. Mwambapa alieleza kuwa wapo wadudu wanaolinda uke,hivyo kemikali inapoingia ndani,husababisha wadudu kupunguza nguvu za kulinda na kuruhusu kemikali kuingia ndani na kuleta madhara.
Mtalamu huyo alishauri wanawake wasiweke vitu vyenye kemikali ndani ya uke,wala kujisafisha na vitu vya aina yoyote vyenye kemikali na wanapaswa kujua kwamba uke huwa unajisafisha wenyewe. Hakuna haja ya kutumia vitu vitakavyoleta madhara makubwa katika uzazi.
USHAURI WA PROFESA JANABI
Kauli hizi za madaktari zinakumbusha ushauri wa Profesa Mohamed Janabi kuhusu mtindo wa maisha. Kwa sasa Profesa Janabi ni Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Kanda ya Afrika, lenye makao yake makuu, Brazaville, Jamhuri ya Congo. Alianza kuutumikia wadhifa huo,mwaka jana.
Profesa Janabi ambaye alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, amekuwa akishauri kwamba ni muhimu kwa jamii kujikita katika kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwa kuwa yana usumbufu na gharama kubwa kuyatibu.
Alisema hajakataza watu kula,bali anachoshauri ni kula kwa kiasi na chakula bora. Suluhu ya magonjwa yasiyoambukiza ni kubadili mtindo wa maisha, kwa kulala sawasawa,kufanya mazoezi, kuongeza ulaji wa mboga mboga, matunda na kupunguza msongo wa mawazo, anashauri.
Mkurugenzi huyo mpya wa WHO Afrika, alifafanua kwamba magonjwa yasiyoambukiza yanasababishwa na mtindo wa maisha, hususan vyakula. Hivyo, kama mtu ana nia anaweza kuondokana na tatizo hilo.
RATIBA YA KULA
Naye Ofisa wa Lishe wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI),Husna Yasin Faraji, alishauri kuhusu muda wa saa za chakula. Anasema mwili wa binadamu unahitaji saa 10 hadi 12,kukaa bila kula chakula cho chote ili kuwa na mwenendo bora wa afya. Alisema mwili wa binadamu unatakiwa kupumzika kwa saa 10 hadi 12,bila kula, ndiyo maana inashauriwa chakula cha usiku kuliwa saa 12 jioni. Mpangilio mzuri wa muda wa kula ni kunywa chai saa 12 asubuhi, chakula cha mchana saa 6(sita) mchana na usiku saa 12 jioni. (Mawasiliano na Mwandishi WhatsApp 0784291434;email nakajumoj@gmail.com).




