Na NASRA KITANA
WAKATI kikosi cha Yanga kikiendelea na maandalizi yake kwa ajili ya mchezo wa kwanza hatua ya makundi wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), uongozi wa timu hiyo umeweka wazi kuwa wachezaji wao wana morari ya kuisambaratisha FAR Rabat ya nchini Morocco.
Yanga inatarajiwa kushuka dimbani keshokutwa katika mchezo wake wa kwanza wa hatua ya makundi utakaopigwa Uwanja New Amaan Complex, Zanzibar kuanzia saa10:00 jioni.
Akizungumza mara baada ya kumaliza mazoezi yao ya kwanza visiwani humo jana, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ally Kamwe alisema hali ya wachezaji wote ipo vizuri na kila mmoja ana morari ya kushinda mchezo huo.
Alisema huo siyo mchezo wa mdogo kwao wanahitaji kuingia na mbinu mbadala ili kuonyesha uwezo mkubwa waliokuwa nao na kupata ushindi wakiwa katika uwanja wa nyumbani.
“Niseme wachezaji wetu wote wana morari ya kutosha kuelekea katika mchezo huo muhimu, kila mmoja anahitaji pointi tatu ili kuweza kutimiza malengo tuliokuwa nayo,” alisema Kamwe.
Ofisa habari huyo alisema huo ni mchezo muhimu kwao na wanahitaji ushindi wa kupata pointi tatu.
Aliwaomba mashabiki na wapenzi wa timu hiyo kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi uwanjani kuwapa sapoti wachezaji wafanye vizuri.
Naye Meneja wa timu hiyo, Walter Harrison alisema wachezaji wote wapo vizuri na wale wa kimataifa ambao walikuwa katika majukumu ya mataifa yao walitarajiwa kujiunga na kikosi hicho jana jioni kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo huo.
Alisema kuwa Kocha Pedro Goncalves anaendelea na programu yake ya mazoezi ambapo timu hiyo inafanya mazoezi asubuhi na jioni.
“Timu imefika salama Zanzibar na mapema imeanza maandalizi kuelekea katika mchezo dhidi ya FAR Rabat na mwalimu ametoa programu ya mazoezi ambapo itafanya mazoezi mara mbili kwa siku asubuhi na jioni,” alisema Walter.
Katika mashindano hayo Yanga ipo kundi B ikiwa na timu za Al Ahly ya Misri, FAR Rabat ya Morocco na JS Kabylie ya Algeria.




