Na MWANDISHI WETU
KATIBU wa NEC Itikadi, Uenezi, na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema heshima ya CCM ni kubwa kuliko fedha na umaarufu, hivyo maamuzi ya chama juu ya wagombea hufanywa kwa kuangalia uadilifu na maadili ya mgombea husika.
Kihongosi ameeleza hayo akizungumza na wananchi wa Kata ya Nyehunge Halmashauri ya Buchosha Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza, ikiwa ni muendeleo wa ziara yake Kanda ya Ziwa.
Kihongosi ameeleza hayo akijibu hoja ya moja wa wananchi, Leonard Methusela iliyeuliza kwanini ngazi za juu za chama zinawakata wagombea ambao wamepitishwa na wajumbe na kuleta majina ya watu wanao wataka wao, hatua ambayo inawagombanisha wananchi na wagombea wao.
Akijibu hoja hiyo Kihongosi amesema majina ya wagombea yanapochujwa huanza kutoka ngazi ya chini na kuendelea hadi Halmashauri Kuu ya Taifa,lakini kuna baadhi ya vitu wakiona si sawa huwa wanawakata ili kuweka wanaofaa.
Amesema chama hakimpi mtu nafasi kwa sababu wanaamini ana nguvu ya fedha au umarufu ndani ya CCM ,hawaangalii vitu hivyo bali wanaangalia heshima ya chama, na kuongeza kuwa wakiendekeza hela, rushwa au kujuana wengi wasingepata nafasi hata yeye asingekuwa mwenezi wa chama.
“Wale wanaotoa rushwa au kujaribu kuathiri mchakato wa uteuzi hawataweza kuleta maendeleo. Heshima ya Chama Cha Mapinduzi ni kubwa kuliko mali au umaarufu wa mtu,” amesema Kihongosi.
Ameongeza; “Tukiendekeza fedha, rushwa au uhusiano binafsi, hata mimi leo nisingekuwa Mwenezi wa CCM, hii ni kwa sababu heshima na nidhamu ya chama ndiyo msingi wa uteuzi wa viongozi”.
Amesisitiza uteuzi wa viongozi ndani ya chama hicho lazima uende sambamba na heshima, uadilifu na kupinga rushwa ili kuhakikisha maendeleo endelevu kwa wananchi, lakini wamekuwa wakibaini kuna wengi wamekuwa wakipita kwa njia zisizo halali.




