NA MUSSA YUSUPH, DODOMA
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amewashusha presha vigogo wa serikali kuhusu mkeka wa uteuzi kutoka kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, huku akitoa onyo kwa watumishi wa umma wanaoacha kutekeleza majukumu kwa madai ya kusubiri uteuzi.
Dk. Mwigulu alisema wanaoacha kufanyakazi kwa kisingizio cha kusubiri uteuzi, ndiyo watakaokumbwa na panga la uteuzi ambapo alitoa msisitizo kwa wakuu wa mikoa, makatibu tawala na wakurugenzi wa halmashauri kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Akizungumza jijini hapa, alipofunga kikao cha kuhakiki Rasimu ya Pili ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II) Dk. Mwigulu, alisema wanaoacha kufanyakazi kusubiri mkeka, utawakumbuka.
“Ipo minong’ono katika baadhi ya maeneo watu wanasubiri mkeka. Hilo ni jambo ni baya japo kuwa tunaamini ukishazaliwa kuna kufa, lakini hatusubiri kufa. Ukisubiri mkeka utakukumba tu kwa sababu utaacha kazi, Rais Dk. Samia alishasema hii serikali inaendelea kwa kipindi cha pili watu wachakarike wachapekazi.
Amesisitiza: “Fanyakazi kwa sababu kazi ndiyo itakayokuweka kazini, ukiacha kazi ndiyo itakayokutoa kazini, ambizaneni wote mchape kazi. Rais anaridhishwa na kazi mnazofanya.”
Aidha alisema mpango huo ni maalumu umeanzishwa ili kuvutia mazingira ya biashara kila sekta, kuweka mazingira wezeshi, kuondoa vikwazo vilivyosalia vya biashara, kupunguza gharama za ufanyaji biashara na kupunguza muda wa upatikanaji huduma.
“Nchi imelenga kufikia uchumi wa kati ngazi ya juu mwaka 2050, hivyo lengo hilo litaweza kutimia kama tutaboresha ufanyakazi, biashara, uwekezaji na ushirikishwaji wa sekta binafsi,” ameeleza.
Amesema takwimu zinaonesha mwaka vijana zaidi ya milioni moja wanaingia katika sekta ya ajira, hivyo bila kuishirikisha na kuikuza sekta binafsi ni vigumu kutengeneza ajira kwa kundi hilo.
Amesema serikali imeonesha nia na utashi wa kisiasa kwa kuwa Rais Dk. Samia, ametekeleza hatua mbalimbali katika kuwekeza kwenye miundombinu, nishati na TEHAMA.
Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema moja ya eneo ambalo limekuwa kikwazo ni uwepo wa taasisi nyingi za usimamizi ambazo zimekuwa kikwazo kwa biashara.
Profesa Kitila amesema wizara yake imeandaa mapendekezo namna ya kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji kwa kuondoa utitiri wa taasisi za usimamizi nchini ambazo zimekuwa kikwazo kwa ukuaji biashara.
Waziri huyo alisema Julai 17 mwaka jana wakati Rais Samia akizindua Dira ya Taifa ya Maendeleo, alitoa maagizo kwa wizara kuandaa mikakati ya kutekeleza dira hiyo.
Amesema moja ya mikakati waliyojiwekea ni kupitia upya MKUMBI huku wizara yake na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI ikiaandaa nyezo za upimaji kila mkoa ili kubaini namna wanavyowezesha biashara na kuvutia uwekezaji.
Kwa upande wake, Waziri wa Fedha, Balozi Mussa Amir Omar, alisema matumaini katika utekelezaji wa Dira 2050 ni kufikia uchumi wa dola trilioni moja katika kipindi cha miaka 25 ijayo.
Amesema katika kufikia lengo hilo hakuna sababu ya kufanyakazi kwa mazoea kwani watumishi wa umma wanapaswa kufanyakazi kwa pamoja ili kufikia mageuzi makubwa ya kiuchumi.
Kuhusu sekta ya fedha, alisema kuna mifumo ya kisheria, fedha na kikodi ambayo Rais Dk. Samia alishaunda tume maalumu kuangalia mfumo wa kodi ambapo MKUMBI II na matokeo ya tume hiyo yatasaidia kutekeleza mikakati ya serikali.
Akiwakilisha wakuu wa mikoa, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima, amesema wapo wawekezaji wazawa wa kigeni na wawekezaji wachanga ambao wanapaswa kupewa nafasi ya kukuza biashara zao hatimaye kuwa wafanyabiashara wakubwa nchini.
Mbunge wa Muleba Kusini, Dk. Oscar Kikiyo, akimwakilishwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Utawala, Katiba na Sheria, alisema sheria nyingi zinazokuja badala ya kulipeleka mbele Taifa linarudisha nyuma kwani zinaongeza nguvu zaidi upande wa serikali badala ya sekta binafsi.




