Na NASRA KITANA
SAA chache mara baada ya Rais wa Yanga Mhandisi Hersi Said, kukutana na Kocha mpya wa timu hiyo, Manqoba Mngqithi na kufanya kikao cha kwanza na benchi zima la ufundi, uongozi wa timu hiyo umesema unajivunia kumpata kwani wana imani watabeba mataji mengi msimu ujao.
Julai 10, mwaka huu Yanga ilimtambulisha kocha huyo akirithi mikoba ya aliyekuwa kocha wao Pedro Goncalves waliyeachana naye Mei 6, mwaka huu.
Yanga waliachana na Pedro baada ya kutoridhishwa na mwenendo wa timu kwa baadhi ya mechi na kikosi hicho alikabidhiwa Kocha wa Msaidizi, Abdihamid Moallin kumalizia mechi 10 zilizobakia msimu huu uliomalizika.
Moallin alisimamia vyema timu hiyo na kufanikiwa kuchukua ubingwa wa tano mfululizo wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kumalizia ikiwa na pointi 75 huku wapinzani wao Simba wakimaliza nafasi ya pili kwa pointi 73.
Akizungumza mara baada ya kocha huyo kukutana na uongozi wa Yanga jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa timu hiyo Ally Kamwe alisema tayari kocha na wasaidizi wake walishawasili na kuingia kambini moja kwa moja kuanza programu za msimu mpya utakaoanza mwezi ujao.
Alisema kuwa kocha huyo amekuja mapema nchini ili kuanza maandalizi ya haraka ya msimu ujao na kutimiza malengo ambayo amepewa na uongozi.
Alisema wanajivunia kumpata kocha huyo na kwamba wana imani atawasaidia kufanya vyema ikiwemo kubeba mataji mbalimbali kuanzia msimu ujao.
“Kocha ameshawasili na leo (jana), amekutana na Rais Hersi akiwa na benchi zima la ufundi.
“Walikaa kikao cha muda mchache na uongozi na uongozi kupanga mikakati mbalimbali ya msimu ujao.
“Baadaye alipelekwa moja kwa moja kambini kuonana na wachezaji na kuanza programu zake, tuna matumaini makubwa tutafanya vyema ikiwemo kubeba mataji mbalimbali chini yake,” alisema Kamwe.
Benchi jipya la timu hiyo linaundwa na Kocha Mngqithi akisaidiana na Simo Dladla.
Pia, Yanga imemtangaza Kocha wa Makipa, Greg Etafia kutoka Nigeria vilevile imefanikiwa kumchukua Mtaalamu wa Uchambuzi wa Viwango na Mifumo ya Soka, Yardaan Valodia.
Hadi hivi sasa, Yanga imewasajili nyota wapya wawili ambao ni Hussein Mihambo na Abdulnasir Mohamed wote kutoka Mashujaa FC ya Kigoma.




