Na NASRA KITANA
UONGOZI wa klabu ya Simba, umemwongeza mkatababa wa mkopo wa mwaka mmoja mshambuliaji wake Selemani Mwalimu ambapo ataendelea kuwepo kikosini hadi mwishoni mwa msimu ujao.
Pia umekanusha kumuuza staa wake Libasse Gueye na Anicet Oura, hivyo wataendelea kuwepo kikosini kwa kipindi kirefu.
Mwalimu ataendelea kuwa sehemu ya kikosi hicho, baada ya Simba kufikia makubaliano na timu ya Wydad AC ya Casablanca inayommiliki nyota huyo.
Simba imefikia uamuzi huo baada ya kuridhishwa na kiwango cha Mwalimu msimu uliopita ambapo aliifungia timu hiyo jumla ya mabao 15 katika mashindano yote.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja wa Habari na Mawasiliano Simba, Ahmed Ally alisema kuwa wasingeweza kumuacha Mwalimu kutokana na uwezo mkubwa ambao aliuonyesha katika kikosi chao msimu uliopita.
Alisema ili kuweza kuendelea kufanya vizuri msimu ujao ni lazima kuwa na mchezaji kama Mwalimu ndiyo maana Simba wameamua kuendelea kuwa naye.
“Mwalimu ataendelea kusalia Simba, baada ya kufikia makubaliano na kumwongeza mkataba wa mwaka mmoja kucheza kwa mkopo hadi mwishoni mwa msimu ujao.
Pia kuna taarifa kuhusiana na mchezaji wetu, Gueye na Oura kwamba tumewauza kitu ambacho siyo kweli kwani wachezaji hhao bado ni mali ya Simba na watakuwepo kwa muda mrefu,” alisema.
Ahmed alisema tetesi za kuwa wachezaji hao wanaondoka hazina ukweli wowote na kusisitiza kuwa nyota huyo bado wana mkataba na wapo katika mpango wa Kocha Steve Berker kuelekea msimu mpya.
USAJILI WA WACHEZAJI WENGINE
Ahmed alisisitiza kwamba klabu yao bado haijafunga hesabu za usajili kwa ajili ya msimu mpya wa mashindano.
Alisema uongozi umejipanga vizuri kusajili wachezaji wenye uwezo mkubwa na kiu ya kupambana, watakahakikisha klabu hiyo inarudi katika ubora wake na kufanya vizuri katika mashindano yote ya ndani na kimataifa.
“Kipindi cha usajili Simba, tumeshatangaza wachezaji watatu tumewasajili, sababu wameaminiwa na Simba waende wakafanye kazi, sisi ndiyo tunafahamu ubora, thamani na kiwango chao.
“Usajili bado haujakamilika, tunaendelea kusajili na kutambulisha wachezaji wapya, leo (jana) tunapumzika lakini kesho (leo) tunatarajia kumtambulisha mchezaji mkubwa ambaye kila mmoja atamshangaa,” alisema Ahmed.
Hadi hivi sasa, Simba imeshakamilisha usajili na kuwatangaza rasmi wachezaji Nathaniel Chilambo akitokea Azam FC, kiungo Kelvin Nashon aliyekuwa Pamba Jiji na kiungo mshambuliaji Bakari Msimu aliyesajiliwa kutoka Coastal Union ya Tanga.
SAFARI YA RWANDA
Ahmed alisema kikosi cha timu hiyo jana kilitua Rwanda kwa ajili ya michuano ya Kagame ambayo itaanza rasmi kesho nchini humo.
Ahmed alisema kikosi chao kilisafiri na wachezaji 20 wakiwemo Oura, Inocent Loemba, Clatous Chama na wale wapya waliokamilisha kuwasajili.
“Mashindano haya ni muhimu kwetu kueleke msimu mpya wa Ligi Kuu Bara, kwani itakuwa ni moja ya maandalizi yetu na tuna imani kuwa tutakwenda kufanya vizuri na kocha atatimiza malengo yake,” alisema Ahmed.
SIMBA DAY
Wakati huo huo, Ahmed alitangaza kuwa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Simba, ‘Simba Day’ kwa msimu wa 2026/2027 kitafanyika Agosti 8, mwaka huu katika Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam.
Ahmed alisema uamuzi wa kuhamishia tamasha hilo katika Uwanja wa Uhuru umefanyika ili kupisha ukarabati unaoendelea Uwanja wa Benjamin Mkapa kuelekea fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
“Simba Day 2026 itafanyika katika Uwanja wa Uhuru, kutokana na ukubwa wa tamasha hili tulitamani kufanyia Uwanja wa Benjamin Mkapa, lakini kwa sasa upo katika ureshwaji kuelekea AFCON 2027,” alisema Ahmed.
Hata hivyo Ahmed alisema uzinduzi rasmi wa Simba Day ambao awali ulipangwa kufanyika Julai 25, mwaka huu, hivi sasa utafanyika Agosti Mosi, mwaka huu katika Hifadhi ya Ngorongoro jijini Arusha.
Meneja huyo aliongeza kuwa tamasha hilo litakuwa la kipekee kwa kuwa litakwenda sambamba na kumbukumbu ya miaka 90 ya Simba tangu kuanzishwa kwa klabu hiyo huku likifuatiwa na matukio mbalimbali ya kijamii.
Hata hivyo timu hiyo ilitangaza viingilio vya tamsha hilo ambapo kima cha chini ni sh. 20,000, mzunguko na VIP A ikiwa ni sh 100,000 wakati Platinum watalipia sh. 250,000.
Simba Day ya mwaka huu inafikisha miaka 17 tangu kuanzishwa kwake tangu mwaka 2009.




