VATICAN CITY, Vatican
KIONGOZI wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo, amewakemea viongozi wa kisiasa na wa dini wanaotumia imani za kidini kuhalalisha migogoro na vita, kwani kitendo hicho ni kufuru na dhambi kwa Mungu.
Katika ujumbe wake uliotolewa juzi kuelekea Siku ya Amani Duniani ya Kanisa Katoliki, itakayoadhimishwa Januari mosi, 2026, Papa Leo ambaye ni papa wa kwanza kutoka nchini Marekani, hakumtaja kiongozi yeyote moja kwa moja, lakini alitoa wito kwa waumini wote kupinga matumizi mabaya ya dini katika siasa.
“Kwa bahati mbaya, imekuwa kawaida kuona lugha ya imani ikiburuzwa katika mapambano ya kisiasa, kubariki utaifa na kuhalalisha vurugu na mapambano ya silaha kwa jina la dini,” alisema Papa Leo.
Alisema wapo baadhi ya viongozi wa dini ambao wamekuwa wakiitumia kama daraja la kuchochea chuki kwa waumini, huku wao wakitafsiri matukio hayo kama uzalendo, jambo ambalo amelikemea.
Kutokana na hali hiyo, alisisitiza waumini wanapaswa kupinga mwenendo huo kwa vitendo na maisha yao ya kila siku.
“Waumini lazima wapinge kikamilifu, hasa kwa ushuhuda wa maisha yao, aina hizi za kufuru zinazolivunjia heshima jina takatifu la Mungu,” aliongeza.
Katika ujumbe huo wa kurasa nne unaotolewa kila mwaka, Papa Leo, pia alilalamikia ongezeko la matumizi ya kijeshi duniani, akinukuu takwimu za Taasisi ya Stockholm ya Utafiti wa Amani (SIPRI) zinazoonesha matumizi hayo yaliongezeka asilimia 9.4 mwaka 2024 na kufikia jumla ya dola za Marekani trilioni 2.7, sawa na asilimia 2.5 ya Pato la Taifa la Dunia (GDP).
Papa Leo aliyechaguliwa Mei, mwaka huu, baada ya Papa Francis kufariki dunia, aliendelea kuonya juu ya hatari za kutumia dini kama chombo cha kuhalalisha vurugu.
Katika safari yake ya kwanza nje ya nchi kama Papa, aliyoifanya nchini Uturuki mwezi uliopita, aliwaambia viongozi wa Kikristo Mashariki ya Kati lazima wakatae kwa nguvu matumizi ya dini kuhalalisha vita au aina yoyote ya misimamo mikali.




