Na SIMON NYALOBI
WAKATI leo Tanzania inaungana na mataifa mengine kuadhimisha Siku ya Figo Duniani, wagonjwa 3,342 wanaendelea kupatiwa huduma ya uchujaji damu nchini.
Hayo yalisemwa na Mratibu wa Huduma za Figo wa Wizara ya Afya, Dk. Abdi Chaula, alipozungumza na gazeti hili kuhusu ugonjwa wa figo.
Kwa mujibu wa Dk. Chaula kumekuwa na ongezeko la wagonjwa hao kutoka wagonjwa 1,017 waliokuwepo mwaka 2019 hadi kufikia 3,342 mwaka huu.
“Hali ya ugonjwa ilivyo hivi sasa kuna wagonjwa 3,342 wa figo wanaopatiwa huduma ya uchujaji wa damu katika vituo 73 vinavyotoa huduma hiyo kote nchini,”alisema.
Aidha, wagonjwa 177 walipandikizwa figo kupitia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) katika matawi yake ya Upanga na Mloganzila jijini Dar es Salaam na Hospitali ya Benjamin Mkapa ya jijini Dodoma.
Akizungumzia sababu za ongezeko la wagonjwa wa figo nchini, alisema kumetokana na sababu mbalimbali, zikiwemo mabadiliko ya mtindo wa maisha ya watu katika nyanja za ulaji na matumizi ya pombe kupita kiasi.
Dk. Chaula alizitaja sababu nyingine ni kutofanya mazoezi, matumizi makubwa ya chumvi, kutokunywa maji ya kutosha na kutokuwa na utamaduni wa kupima afya kila wakati.
Alifafanua ugonjwa huo hauna tabia ya kuonesha dalili za awali, hali inayosababisha watu wengi kwenda hospitali wakiwa katika hatua za mwisho ya kuathirika.
“Hatuna utamaduni wa kupima afya kila wakati na ugonjwa huo katika hatua za mwanzo hauna dalili hadi hatua ya tano ndiyo huonesha dalili, ambayo tayari ugonjwa unakuwa umefikia pabaya,”alisema.
Alishauri jamii kujenga tabia ya kupima afya angalau mara moja kwa mwaka, hali itakayowasaidia kugundua iwapo wana ugonjwa huo mapema.
Kuhusu jitihada za serikali kukabiliana na ugonjwa huo, alisema serikali imejikita katika kutoa elimu kwa jamii katika kubadilisha mtindo wa maisha kupitia vyombo vya habari.
Alieleza serikali imetoa mwongozo wa mtindo bora wa maisha na mwongozo wa kufanya mazoezi kuepukana na ugonjwa huo.
Aidha, alisema imeongeza wigo wa tiba kuongeza vituo vya tiba ambapo alisema vituo vya tiba vimeongezeka kutoka 17 vilivyokuwa mwaka 2017 hadi 73.
Kwa mujibu wa Chaula, serikali imepunguza gharama matibabu ya uchujaji damu kwa mzunguko mmoja kutoka sh. 250,000 hadi sh. 150,000.




