Dodoma
Na Selina Mathew
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema sauti ya Watanzania imesikika kupitia sanduku la kura katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 29 mwaka, hivyo inapaswa kuheshimiwa.
Dk. Samia aliyasema hayo katika hafla ya ufunguzi wa mwaka mpya wa mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini, Ikulu Chamwino Dodoma.
Alisema demokrasia ni safari ya ukuaji na kwamba kila mfumo wa kisiasa una malalamiko na changamoto zake.
Alibainisha kuwa ni wazi kwamba hakuna kanuni moja ya kidunia ya kutatua changamoto za kipekee, huku akisisitiza ni lazima nchi zipeane nafasi ya kujifunza na kukua kwa unyenyekevu.
“Kwa wale waliotuma ujumbe wa mshikamano na pongezi, tunawashukuru. Kwa wale ambao hawakufanya hivyo, tumepokea maoni yenu pia.
“Nawaomba ninyi marafiki wenye nia njema, muunge mkono mageuzi yetu. Na kwa wale ambao huenda hawashiriki maono yetu, nawaomba angalau muheshimu mamlaka yetu ya kitaifa. Sauti ya Watanzania imesikika kupitia sanduku la kura na sauti hiyo ni lazima iheshimiwe,”alisisitiza.
Rais Dk. Samia alisema Tanzania imefanikisha uchaguzi wa saba wa kidemokrasia uliofanyika Oktoba 29 mwaka jana kwa mafanikio makubwa.
Aliyataja mafanikio hayo ni kwamba uchaguzi huo ulifadhiliwa kikamilifu kupitia rasilimali za ndani jambo linalothibitisha umiliki wa kitaifa, ukomavu wa kitaasisi na dhamira ya serikali kujitegemea katika kusimamia mchakato wa kidemokrasia.
Hata hivyo, alikiri kuwa licha ya uchaguzi kufanyika kwa mafanikio makubwa zilijitokeza changamoto za vurugu na ukosefu wa utulivu siku ya uchaguzi na muda mfupi baadaye.
“Licha ya mafanikio haya makubwa, kwa masikitiko tunatambua changamoto zilizotokea kutokana na vurugu, ukosefu wa utulivu siku ya uchaguzi na muda mfupi baadaye. Hatua tulizochukua zilikuwa muhimu ili kudumisha utaratibu wa kikatiba na kuhakikisha usalama wa wananchi pamoja na jamii ya kidiplomasia,” alisema.
Alisisitiza: “Kwa washirika wetu katika jamii ya kidiplomasia na wageni wanaoishi hapa nchini, ninatoa pole ya dhati kutokana na hali ya kutokuwa na uhakika, usumbufu wa huduma na kufungwa kwa mtandao wa intaneti. Nawaahidi tunakuwa makini kuhakikisha usalama wenu, kuzuia hali kama hiyo kujirudia katika siku zijazo.”
Dk. Samia alisema hatua kubwa za kidiplomasia na kisiasa zinazolenga kuleta uponyaji wa kitaifa na maridhiano baada ya misukosuko ya uchaguzi, zilichukuliwa.
Alizitaja hatua hizo ni sehemu ya mkakati wa serikali kurejesha utulivu na kuimarisha mshikamano miongoni mwa Watanzania.
Rais Samia alisema kupitia mageuzi makubwa ya kiuongozi, alipandisha hadhi masuala ya vijana kwa kuanzisha Wizara ya Vijana chini ya Ofisi ya Rais.
Alisema wizara hiyo mpya ina jukumu la kuratibu nguvu, ari na matarajio ya kizazi kipya cha Watanzania ambacho ni nguzo ya maendeleo ya taifa.
“Tunaelewa makosa ya huko nyuma, lakini macho yetu yamekazwa thabiti kuelekea mbeleni,”alisema na kuongeza kuwa watuhumiwa 1,787 wa vurugu za Oktoba 29 walisamehewa.
Kuhusu mustakabali wa kisiasa, Rais Dk. Samia aliahidi kuanzisha tume ya ukweli na maridhiano ambayo itakuwa msingi kuelekea mchakato wa Katiba mpya.
Alieleza kuwa muhula wa pili utajikita katika kurekebisha, kujenga upya na kuimarisha taifa kwa misingi ya haki na mazungumzo.
Rais Dk. Samia alisisitiza kuwa diplomasia ya uchumi itaendelea kuwa kiini cha sera ya mambo ya nje ya Tanzania.
“Serikali itaongeza nguvu katika uchumi wa buluu na kijani, teknolojia ya kidijitali na usimamizi madhubuti wa rasilimali kama gesi asilia na madini ili kukuza ajira na maendeleo jumuishi kwa wote,” alieleza.
Dk. Samia alitumia nafasi hiyo kuzipongeza serikali mpya zilizochaguliwa katika mataifa jirani huku akisisitiza Tanzania ipo tayari kufanya kazi na serikali hizo ili kuimarisha umoja wa Afrika kuwa na bara lenye ushirikiano na ustawi.
“Tunatambua kwa kuridhika ustahimilivu wa kidemokrasia uliotawala kote duniani, licha ya changamoto zetu wenyewe, tunasherehekea makabidhiano ya madaraka kwa amani yaliyoshuhudiwa katika mataifa rafiki nje ya nchi, ikiwemo baadhi ya nchi zenu,“ alibainisha.
Alisema mafanikio yao yanatoa mwelekeo wa mageuzi ya kitaasisi kwa kuwa diplomasia imejikita kwa kina katika kuheshimiana.
“Natoa pongezi zangu za dhati kwa mataifa yote yanayoadhimisha siku zao za kitaifa mwezi huu, Tanzania inasherehekea nanyi. Maendeleo yenu yanachochea maendeleo yetu, ambapo urafiki ndiyo nguzo ya sera yetu ya mambo ya nje,” alisisitiza.
Alisema Tanzania inabaki kuwa miongoni mwa nchi za Afrika ambazo uchumi wake unakua kwa kasi ukiwa na pato la taifa la asilimia 5.9, huku mfumuko wa bei ukiendelea kudhibitiwa na kubali asilimia 3.3 na pia deni la taifa limeendelea kuwa himilivu kwa asilimia 48.2 chini kiwango cha nchi zenye kipato cha chini ambacho ni asilimia 55.
Aidha alisema kuwa alama bora za kukopesheka na uimara wa uchumi umewezesha Tanzania kuvutia miradi mipya ya uwekezaji 927 hadi kufikia Desemba mwaka jana ikiwa na thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 11.09, ikiwa ni ongezeko la asilimia 19.03 ikilinganishwa na mwaka juzi.
Alisema miradi hiyo inatarajiwa kutoa zaidi ya ajira 162,865 kwa Watanzania, huku miradi ya uwekezaji kutoka nje ikiendelea kushamiri na amewahakikishia wawekezaji miradi iliyopo na mipya italindwa na kuendelea kuwa salama.
WAZIRI MAMBO YA NJE
Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, alisema diplomasia ya Tanzania imepita katika mtihani tangu uhuru kufuatia matukio ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29 mwaka jana ambapo sasa nchi imerejea katika mstari wake.
“Matukio ya uchaguzi uliopita yaliharibu taswira ya nchi (Tanzania) duniani na kuzua maswali mengi kutoka kwa washirika wa maendeleo. Nilipokea simu nyingi na ujumbe wa maandishi wa kutia moyo na mshikamano kutoka kwa marafiki na washirika wetu wengi wa karibu.
“Baadhi walijumuisha wasiwasi pia, huku wengine wakiuliza nini kimeipata Tanzania, nchi inayojulikana kama kitovu cha amani kwa miaka 64 iliyopita tangu uhuru wake. Wengine waliwasilisha ujumbe wao kupitia njia za kidiplomasia kwako Mheshimiwa, huku baadhi isivyo bahati wakitumia majukwaa na maeneo yasiyo rasmi,”alibainisha.
Alisema kuwa chini ya maelekezo ya Rais Dk. Samia, wizara yake ilifanya kazi ya ziada kufafanua ukweli wa mambo kwa kutumia ushahidi katika miji mikuu ya Dunia hatua iliyosababisha nchi kueleweka.
Alieleza kuwa Umoja wa Mataifa (UN) umekubali kutoa nafasi ya uponyaji kupitia Tume ya Uchunguzi iliyoundwa na Rais, ambayo itafuatiwa na mchakato wa maridhiano ya kitaifa.
“Mbinu ya “4R” (Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Kujenga Upya) ya Rais Samia imekuwa nguzo muhimu katika kurejesha imani ya jumuiya ya kimataifa, huku akibainisha kuwa kila sauti ya upinzani au wasiwasi ilisikilizwa na kufanyiwa kazi kwa wakati muafaka,” alibainisha.
MWENYEKITI WA MABALOZI
Naye, Mwenyekiti wa mabalozi nchini na Balozi wa Comoro, Ahmada El Badaoui Mohammed Fakhi, alimpongeza Rais Dk. Samia kwa ushindi wa kishindo katika uchaguzi mkuu, akiahidi kuendelea kuyaishi maono ya Dira ya Maendeleo 2050.
“Tanzania ina nafasi ya kipekee katika bara la Afrika na Dunia sababu ya amani, utulivu na kuwa daraja la biashara na taifa ambalo sauti yake ina nguvu,” alifafanua.
Alisema Tanzania inaendelea kuonyesha dhamira na uwezo wake kupitia amani iliyoimarika wakati ambao Dunia inapitia kipindi kigumu.
“Mataifa mengi huwa yanajaribiwa lakini hushinda nyakati ngumu na kusonga mbele, tulifuatilia yaliyotokea kipindi cha uchaguzi tukaona namna ambavyo serikali ilifanya kazi kudhibiti hali hiyo,” alisema.




