Na MWANDISHI WETU
OFISI ya Makamu wa Rais, imebuka mshindi wa nafasi ya tatu kupitia mchezo wa karata upande wa wanawake katika Mashindano ya Mei Mosi, 2026 yanayoendelea mkoani Njombe.
Mchezaji aliyepeleka shangwe upande wa timu ya Ofisi ya Makamu wa Rais ni Shinuna Mohamed aliyemfunga Annastazia Majenga kutoka Chuo cha Maendeleo ya Mipango Vijijini (IRDP) alama 2-0 katika mchuano uliofanyika Uwanja wa CCM Sabasaba mwishoni mwa wiki.
Akizungumzia ushindi huo, Shinuna aliishukuru menejimenti ya Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kuthamini michezo na kusema mafanikio hayo yawahusu watumishi wote.
Alisema ushindi huo ni historia kwake ikizingatiwa ilikuwa mara yake ya kwanza kushiriki mashindano makubwa ya karata, ambayo alipaswa kutumia mbinu za ziada kuwafunga wapinzani wake.
“Timu zote zimejiandaa vyema na mashindano haya, nilitumia uzoefu wangu kwa kusoma mbinu za wapinzani na kuweza kuwafunga…Ninajivunia mafanikio haya, naahidi kuweka bidii zaidi mashindano yajayo nishike nafasi za juu,” alisema Shinuna.
Aidha, mchezaji huyo alisema mchezo wa karata ni mgumu kama ilivyo mpira wa miguu, ambapo inahitajika maandalizi ya kutosha kupata matokeo mazuri.
Shinuna alisema amefurahia kukutana na wachezaji wazoefu wa mashindano makubwa ikiwemo SHIMIWI, ambao walimfanya atumie akili nyingi kuwashinda katika mchezo wa karata.
Kwa upande wake, Katibu wa Klabu ya Michezo Ofisi ya Makamu wa Rais, Marwa Nyaisawa alieleza ushindi wa Shinuna ni kielelezo cha ari, mshikamano na juhudi zinazoendelea kuoneshwa na wachezaji wa kikosi kizima cha Ofisi ya Makamu wa Rais katika mashindano ya Mei Mosi mwaka huu.
“Tumekuwa na mwendelezo mzuri wa timu yetu katika mashindano ya Mei Mosi pamoja na kushiriki mara ya kwanza, hii inadhihirisha dhamira tuliyojiwekea ya kupata mafanikio tuliyodhamiria,” alisema Nyaisawa.
Alisema mashindano ya Mei Mosi mwaka huu yamewapa uzoefu kwa mashindano mengine baadaye.
Nafasi ya kwanza katika mchezo wa karata kwa upande wa wanawake imekwenda kwa Malkia Nondo kutoka timu ya Mahakama, huku kwa wanaume ikichukuliwa na Susu Jeremia wa kikosi cha Wizara ya Afya.




