Na NASRA KITANA
TIMU za soka za Simba na Mlandege zinatarajiwa kupambana katika mchezo wa Nusu Fainali ya Kombe la Muungano utakaopigwa Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar kuanzia saa 2:15 usiku.
Katika mashindano hayo, Mlandege FC ndio walianza kutinga hatua ya nusu fainali baada ya kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars, wakati Simba ilitinga hatua hiyo baada ya kuichapa bao 1-0 timu ya Mafunzo FC mechi zote zilipwa Uwanja wa New Amaan Complex.
Kuelekea pambano hilo, kocha wa Simba, Steve Barker alisema timu yao imejipanga vizuri kuhakikisha wanapata ushindi.
“Maandalizi kwetu yamekamilika na wachezaji wangu wote wapo tayari kwenda kufanya kila kilichokuwa bora katika mechi hii, ingawa tunafahamu tunakwenda kucheza na timu yenye mafanikio hapa Zanzibar,” alisema Barker.
Nyota wa Simba, David Kameta alisema kama wachezaji watahakikisha wanapambana mwanzo mwisho kupata ushindi na kutinga fainali.
“Nia yetu wachezaji ni kwenda kuchukua ubingwa, ila maandalizi yetu ni mazuri na yanatosha kushinda mchezo wa kesho (leo) pamoja na taji hili,” alisema Kameta.
Kocha Msaidizi wa Mlandege FC, Sabri Ramadhan China, alisema wachezaji wote wapo vizuri na wamejipanga kufanya vyema.
“Wachezaji wangu wapo vizuri na wameniahidi kujituma kadri ya uwezo wao, na mimi nimewapa mbinu nzito,” alisema China.




