Na AMINA KASHEBA
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ametoa neno kwa Watanzania kutoibeza nchi yao kwa sababu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anafanya mambo mazuri yakiwemo maandalizi ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika ‘AFCON 2027’ na kutunza amani ya nchi.
Akizungumza Dar es Salaam, katika pambano la ‘Knockout ya Mama’ msimu wa nane, lililofanyika Ukumbi wa Biashara na Usafirishaji wa Afrika Mashariki, Ubungo Dar es Salaam, alisema kuna baadhi ya watu wakiona AFCON 2027 inafanyika nchini wanaanza kuongea mambo mabaya juu ya taifa.
“Watanzania tunapaswa kuachana na tabia ya kuibeza nchi yetu kwani Rais Dk. Samia anafanya makubwa anatuletea michuano ya AFCON mwakani, pia ‘Miss World’ itafanyika hapa nchini.
“Mashindano haya yatadumu ndani ya siku 28 kwa kufanyika mashindano madogo madogo hadi fainali,” alisema.
Aidha, Waziri huyo alisema Watanzania wanapaswa kufahamu amani ndiyo kila kitu katika nchi, hivyo wanapaswa kuilinda na kuitunza.
“Amani itawale kwani ni silaha kubwa hapa nchini, pia kujiandaa na matukio makubwa ya kimataifa ambayo yatalitangaza taifa letu vizuri na kupata fursa nyingi kupitia mashindano hayo,” alisema.
Wakati huo huo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ametoa maagizo kwa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kuhakikisha mchezo wa mieleka unafanyika kwa ustadi mkubwa.
Maagizo hayo ameyatoa juzi katika pambano la ‘Knockout ya Mama’ msimu wa nane uliofanyika Ukumbi wa Biashara na Usafirishaji wa Afrika Mashariki, Ubungo Dar es Salaam.
Makonda alisema BMT inatakiwa kuhakikisha mchezo wa mieleka unafanyika hapa nchini huku idadi kubwa ya Watanzania wakishuhudia.
“Tanzania ina watu wenye miili mikubwa, hivyo miili yetu tuitendee haki, lazima kila mtu katika hii nchi awe na mchezo wake, hamasa kubwa tumeona katika ngumi tunaomba wasichoke waendelee kuwaleta mabondia kukuza vipaji, “alisema.
Waziri huyo alisema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa mwanamichezo namba moja kwa kugusa kila sekta ya michezo kuanzia soka,riadha, netiboli, ngumi, na michezo mingine amefanya hivyo.
“Nimetoa maagizo mengine kwa Kamisheni ya Ngumi ya Kulipwa (TPBRC),waende nchi nzima kutafuta vipaji na kutambulika na kupanda katika majukwaa makubwa kama haya.




