Na Mwandishi Wetu, Unguja
MAKAMU wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, ametoa wito kwa wakazi wa Dunga, Mkoa wa Kusini Unguja, kuendelea kushirikiana na Idara ya Uhamiaji na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, katika kuhakikisha amani inaendelea kushamiri nchini.
Balozi Nchimbi alitoa wito huo katika hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar katika hafla iliyofanyika katika eneo la Dunga.
Dk. Nchimbi aliwasihi kushirikiana na Serikali kwa njia ya kutoa taarifa mbalimbali kuhusu wahamiaji haramu, watu wanaoishi nchini kinyume cha sheria, au wanaojihusisha na shughuli haramu kinyume na malengo ya ukaazi wao.
Makamu wa Rais alisema amani na umoja ni Tunu za Taifa, ambazo kila Mtanzania anapaswa kuzilinda.
KUMUUNGA MKONO RAIS
Balozi Nchimbi aliwasihi wananchi wote kuendelea kuunga mkono juhudi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, kwa jitihada kubwa wanazozifanya katika kuiletea nchi maendeleo ili kwa pamoja kufikia malengo ya kuboresha maisha ya kila Mtanzania.
Halikadhalika, Makamu wa Rais alitoa rai kwa taasisi za serikali kuendelea kuwaamini na kuwapa Watanzania wazawa kazi za ujenzi, waendelee kupata uwezo wa kiteknolojia na kifedha.
Makamu wa Rais aliipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya uhamiaji, kwa kutoa kandarasi kwa Mtanzania mzawa katika ujenzi wa jengo la Ofisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati, Unguja.
Aidha, alisema Serikali imejikita katika kuimarisha huduma za uhamiaji kwa kuboresha vitendea kazi na miundombinu kwa ujumla.
Dk. Nchimbi aliongeza kuwa, Ujenzi wa Ofisi za Uhamiaji za Wilaya ni njia mojawapo ya jitihada za kufikia azma hiyo.
UBORESHAJI
Pamoja na uboreshwaji wa miundombinu ya majengo, Serikali imeweka mkazo katika utoaji wa mafunzo kwa watumishi, kusimamia stahiki za watumishi, na uboreshaji wa mara kwa mara wa Sheria na Kanuni za Uhamiaji nchini.
Vilevile, alisema huduma za uhamiaji Zanzibar ni muhimu na chachu katika kukuza sekta ya biashara, uwekezaji na utalii, kwa kuzingatia ongezeko kubwa la wageni wanaoitembelea, hususan katika kipindi ambacho Serikali zote mbili zimejikita kukuza sekta ya utalii kufuatia uzinduzi wa Filamu maarufu ya Royal Tour.
MUUNGANO, MAPINDUZI
Makamu wa Rais alisema Mapinduzi ya mwaka 1964, yaliyoongozwa na Rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati Abeid Amani Karume yana historia kubwa kwa Zanzibar na watu wake.
Tangu wakati huo, Mapinduzi hayo yameijengea heshima kubwa Zanzibar na kuwapa Wazanzibari wigo mpana wa kufanya uamuzi kuhusu maisha yao na kujiletea maendeleo.
Pia, alisema Muungano umeimarisha zaidi umoja, mshikamano na kudumisha amani, utulivu na kuchochea maendeleo kwa wananchi wote.
Alisema baada ya Mapinduzi na Muungano, huduma mbalimbali za jamii kama vile afya na elimu zilifunguka kwa wananchi wote.
Jengo hilo la Ofisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati limegharimu sh. bilioni 2.1.





