Na SELINA MATHEW, DODOMA
SERIKALI imewataka washiriki wa shindano la Miss World Tanzania kubeba taswira halisi ya Mtanzania kwa kuzingatia tamaduni, maadili na utu wanapoiwakilisha nchi kimataifa.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda jijini Dodoma alipozungumza na waandishi wa habari kuelekea shindano hilo litakalofanyika Aprili 19, mwaka huu.
Makonda alisema mshiriki atakayechaguliwa kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss World nchini Vietnam, anapaswa kuwa balozi wa heshima ya taifa, akisisitiza kuwa ushindani huo si wa urembo wa sura pekee bali unaangalia mchango wa mshiriki kwa jamii.
Alisema ni muhimu kwa washiriki kuonyesha nidhamu, kujiamini na kulinda maadili ya Kitanzania.
Aliwataka washiriki 20 wanaowania taji hilo kutokata tamaa na kuendelea kupambania ndoto zao, akibainisha kuwa wanawakilisha si familia zao tu bali taifa zima.
“Mashindano haya Tanzania imeshiriki kwa miaka 29 na safari hii ikiwa ni ya 30 tunatarajia kufanya vizuri zaidi. Aidha, mshiriki wetu anapaswa kutangaza Kiswahili, ambacho ni fahari ya Taifa,” alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miss World Tanzania, Mustafa Hassanali, alisema mshindi wa mwaka huu atanufaika na zawadi mbalimbali ikiwemo tiketi ya ndege kwenda Vietnam, gari, sh. milioni 10 pamoja na mshahara wa sh. milioni mbili kwa mwaka mmoja.
Aliongeza kuwa, mshindi huyo atapata nafasi ya kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss World yatakayofanyika Septemba 2026 nchini Vietnam, huku akiahidi ushindani mkali na wa viwango vya juu mwaka huu.




