Na ATHNATH MKIRAMWENI
JUMLA ya watahiniwa 1,172,279 wa darasa la saba, wamesajiliwa kufanya mtihani wa kumaliza Elimu ya Msingi, unaoanza leo, kwa siku mbili mfululizo katika shule 19,441.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Profesa Said Mohammed, alisema jumla ya watahiniwa 1,172,279, wamesajiliwa kufanya mtihani huo huku wavulana ni 535,138, sawa na asilimia 45.65 na wasichana 637,141 sawa na asilimia 54.35.
Watahiniwa hao, wanatarajia kufanya mtihani leo na kesho, asilimia 93.35, watafanya mitihani kwa kiswahili, huku asilimia 6.65, wakifanya lugha ya kiingereza ambayo inatumiwa katika baadhi ya shule binafsi.
Pia, watahiniwa 4,679 wenye mahitaji maalumu, wamesajiliwa wakiwemo wasioona (92), wenye uoni hafifu(1,551), uziwi (1,079), ulemavu wa akili (448) na ule wa viungo (1,509)
“Maandalizi yote muhimu yamekamilika, zikiwemo karatasi za mitihani, vifaa vya kujifunzia kwa watahiniwa wenye mahitaji maalumu na semina kwa wasimamizi,” alisema Profesa Mohamed.
Profesa Mohamed, alisema jumla ya masomo sita, yatapimwa ambayo ni Kiswahili, Lugha ya kiingereza, Hisabati, Sayansi na Teknolojia, Maarifa ya Jamii na Stadi za Kazi, Uraia na Maadili.
Alibainisha kuwa, mtihani huo ni muhimu siyo kwa wanafunzi, bali jamii nzima kwa kuwa, hutumika kupima uelewa wa masomo waliyojifunza na kuamua nani anayeendelea na elimu ya sekondari.
Alitoa wito kwa kamati za mitihani, kuhakikisha usalama katika vituo vya mitihani na kufuata miongozo.
Pia, wasimamizi wa mitihani, wametakiwa kuwa waadilifu, kufuata kanuni na kuhakikisha mazingira ya mtihani ni tulivu.
“Watahiniwa wenye mahitaji maalumu, watapatiwa huduma stahiki, kama vile mitihani ya nukta nundu kwa wasioona na maandishi makubwa kwa wenye uoni hafifu, pamoja na muda wa ziada wa dakika 20 kwa kila saa katika somo la hisabati na dakika 10 kwa masomo mengine,” alisema.
Kwa upande wa watahiniwa, Baraza liliwataka kujiepusha na vitendo vya udanganyifu na kusisitiza kuwa, yeyote atakayebainika, kuhusika atachukuliwa hatua kali ikiwemo kufutiwa matokeo kwa mujibu wa kanuni za mitihani.
Kuhusu wamiliki na wakuu wa shule, walionywa dhidi ya kuingilia majukumu ya wasimamizi wa mitihani, kupewa angalizo kuwa, kituo chochote kitakachobainika kuhatarisha usalama wa mtihani kitaondolewa.
Profesa Mohamed, alitoa wito kwa jamii kwa ujumla, kurikiana kuhakikisha mtihani unafanyika katika mazingira ya amani na utulivu.
UPIMAJI DARASA LA PILI
Profesa Mohamed, alieleza sababu za kufanyika upimaji wa darasa la pili kwa lengo la kuondoa changamoto ya wanafunzi kushindwa kusoma na kuandika.
“Utaratibu wa uendeshaji, utakuwa wa nchi nzima na maswali yatakuwa yanafanana na walimu wanaowafundisha, ndiyo watawasimamia, kusahihisha na kuleta taarifa za matokeo NECTA yatakayosadia kufanyika uchambuzi.




