Na NASRA KITANA
UONGOZI wa Klabu ya Yanga umeziomba timu zote zinazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi ya Championship, kuiombea timu yao, ifuzu hatua ya robo fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL).
Yanga inatarajiwa kushuka dimbani keshokutwa katika mchezo wa mwisho hatua ya makundi ya CAFCL dhidi ya JS Kabylie ya Algeria utakaochezwa katika Uwanja wa New Amaan Complex, visiwani Zanzibar kuanzia saa 1:00 usiku.
Timu hiyo yenye Makao Makuu yake mitaa ya Twiga na Jangwani, inahitaji ushindi wa tofauti ya mabao mawili mbele ya Kabylie, iliyopoteza tumaini la kusonga mbele kupitia kundi B linaloongozwa na Al Ahly ya Misri ikiwa na pointi tisa.
Katika msimamo nafasi ya pili inashikiliwa na AS FAR yenye pointi nane, Yanga nafasi ya tatu kwa pointi tano huku Kabylie ikiburuza mkia ikiwa na pointi tatu.
Akizungumza jijini Dar es Salaam kabla ya kwenda Zanzibar, Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe, alisema kwa hali iliyopo hivi sasa hakuna timu nyingine nchini ambayo angalau ina uhakika wa kusonga mbele hatua ya makundi isipokuwa Yanga pekee.
“Tunaomba timu zote watuombee ili Yanga iheshimishe Tanzania, angalu kama nchi tuwe na timu moja katika hatua ya robo fainali katika michuano ya kimataifa,” alisema Kamwe.
Ofisa huyo alisema kuwa timu yao haitakuwa na mapumziko na badala yake inaendelea na maandalizi kwa ajili ya mechi yao ya mwisho dhidi ya JS Kabylie.
Alifafanua kuwa hawana hofu na timu yao kwani wanakwenda kucheza uwanja ambao wameuzoea, hivyo watapambana mwanzo hadi mwisho kusaka ushindi.
Kamwe alisema kuwa wachezaji wote wana morari ya kutosha kuelekea katika mchezo huo muhimu kwani lengo kubwa ni kupata ushindi wa mabao mengi na hilo linawezekana.
“Niwaambie tu mashabiki na wapenzi wa timu yetu wanatakiwa kujaa kwa wingi uwanjani ili kuweza kuisapoti timu yao na kuwaongezea morari wachezaji wanapokuwa uwanjani,” alisema Kamwe.




